NA CHARLES WASONGA
SHIRIKA la ndege nchini Kenya Airways (KQ) limetangaza kuwa kutakuwa na hitilafu katika safari zake ndani ya wiki mbili kutokana na changamoto ya ukosefu wa vipuri kote ulimwenguni.
Kupitia taarifa, Afisa Mkuu Mtendaji wa shirika hilo Alan Kilavuka, alisema kuna uhaba mkubwa wa vipuri vya ndege katika masoko ya ulimwengu.
“Kutokana na hali hii, baadhi ya ndege zetu zitakaa kwa muda mrefu kwenye maegesho zikisubiri kuletwa kwa vipuri kutoka ng’ambo ndiposa zianze kazi,” akasema.
“Tutalazimika kuchukua hatua hii, isiyoepukika kwa sababu ya kujitolea kwetu kuzingatia usalama na uaminifu katika shughuli zetu,” Bw Kilavuka akaongeza.
Afisa huyo alisema KQ itakuwa ikitoa habari kila mara kwa wateja kuhusu hali hiyo.
“Kwa hivyo, tunaomba wateja wetu na washirika wengine kutizama mitandao yetu ya habari kila mara ili kupata ufahamu kuhusu suala hili na masuala mengine yanayohusu shughuli zetu,” Bw Kilavuka akaongeza.
Changamoto hiyo huenda ikaaathiri mapato ya shirika hilo wakati huu wa msimu wa sherehe za Krismasi na Mwaka Mpya ambapo idadi ya wateja imeongezeka.