• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Mke wake Mwanamfalme adai alibaguliwa sababu ya rangi

Mke wake Mwanamfalme adai alibaguliwa sababu ya rangi

Na MASHIRIKA

LONDON, Uingereza

MKE wa Mwanamfalme wa Uingereza Harry, Meghan Markle, amefichua kuwa karibu ajitie kitanzi baada ya kubaguliwa na familia ya Kifalme kwa kuwa na ngozi nyeusi.

Meghan pia alifichua kuwa familia ya Malkia wa Uingereza Elizabeth ilimchukia na mara nyingi ilitoa madai ya uongo dhidi yake kwa lengo la kumharibia sifa.

Katika mahojiano na runinga yaliyofanywa na mwanahabari na muigizaji maarufu nchini Amerika Oprah Winfrey, Meghan alisema ubaguzi huo ulimfanya yeye na mumewe kukataa majukumu ya kifalme na kuamua kuhamia nchini Amerika.

Baba ya Meghan ni mzungu na mama yake ni wa asili ya Mwamerika Mweusi.

“Sikutamani kuendelea kuwa hai tena. Kila mara niliwazia kujiua baada ya madai ya uongo dhidi yangu kusambazwa mitandaoni na watu ambao hawakunitakia mema,” akasema.

Miongoni mwa madai yaliyomkabili ni kwamba alidhulumu mfanyakazi wake ndani ya Kasri la Kifalme.

Meghan, 39, pia alisema kuwa mwanawe, Archie, alitishiwa kunyimwa cheo katika ufalme huo na kupunguziwa walinzi kwa kuwa ngozi yake ilikuwa nyeusi.

Harry na mkewe Meghan, mnamo Januari 2020 walishangaza ulimwengu walipotangaza kuachana na majukumu yao ya ngazi ya juu katika familia ya kifalme.

Badala yake, wanandoa hao walihamia Amerika ya Kaskazini kuanza maisha mapya.

Kupitia taarifa yao, wawili hao walisema kuwa wataendelea kumuunga mkono kikamilifu Malkia Elizabeth.

“Baada ya miezi mingi ya kutafakari na majadiliano ya ndani, tumeamua kufanya mabadiliko mwaka huu kwa kuanza kutekeleza jukumu jipya ndani ya taasisi hii”, alisema Harry ambaye yuko katika nafasi ya sita katika orodha ya warithi wa kiti cha Ufalme.

Katika mahojiano yaliyopeperushwa jana na runinga ya CBC News, Meghan alisema kuwa hata wakati mmoja aliwahi kuulizwa: “Rangi ya mtoto wako aliye tumboni ni gani?”

“Kabla ya kujifungua mtoto wangu wa kwanza, kila mara nilikejeliwa kuwa nikizaa mtoto mwenye ngozi nyeusi hatapewa cheo katika ufalme na usalama. Hayo yote niliambiwa na Harry kila mara familia ilipojadili suala la rangi ya ngozi ya mtoto,” akasema Meghan.

Baada ya wanandoa hao kuhamia Amerika Kaskazini, baadhi ya vyombo vya habari nchini Uingereza vilishambulia Meghan kwa kumtupia kila aina ya matusi kwa ‘kupotosha’ Harry.

Inadaiwa kuwa Winfrey aliuzia runinga ya CBS mahojiano hayo kwa Sh900 milioni.

Katika mahojiano hayo, wanandoa hao walifichua kuwa wanatarajia mtoto wa kike ambaye atazaliwa hivi karibuni.

You can share this post!

Musalia arai Oparanya ahamie upande wake

TAHARIRI: Matatizo ya CBC yatatuliwe upesi