• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 6:50 AM
Papa Francis ahubiri msamaha, maridhiano

Papa Francis ahubiri msamaha, maridhiano

NA MASHIRIKA

KINSHASA, DRC

KIONGOZI wa Kanisa Katoliki duniani Papa Francis, mnamo Jumatano aliwasihi raia wa Congo kuwasamehe wale waliowakosea.

Alisema hayo alipokuwa akiongoza misa iliyohudhuriwa na watu takriban milioni moja waliofurika, tukio ambalo ni kubwa la kwanza la Papa Francis barani Afrika.

Aidha, lengo kuu la ziara ya Papa ni kuleta amani na maridhiano kwa nchi iliyoathiriwa na ghasia kwa miongo kadhaa.

Mbali na hayo, waumini wengi wa Congo walikesha wakisubiri misa kwenye viwanja vikubwa kwenye uwanja wa ndege wa Ndolo wakisubiri kuwasili kwa Papa Francis.

Papa Francis akiwa na Rais wa DRC Felix Tshisekedi. PICHA | AFP

Waliimba na kucheza wakiwa wamejawa na msisimko juu ya ujio wa kwanza wa Papa tangu Mtakatifu John Paul wa Pili alipofanya ziara yake ya mwisho mwaka 1985.

Walishangilia wakati Papa huyo alipoanza kuzunguka taratibu kwenye viwanja vya wazi akiwa katika gari lake la kipapa baadhi yao wakikimbia kando yake au kupeperusha bendera.

Wanawake wengi walikuwa wamevalia magauni na sketi zilizoshonwa kwa vitenge vya waksi vyenye picha ya Papa Francis au alama nyingine za kidini.

“Leo ninaelewa furaha ya nyanya yangu wakati Papa John Paul II alipokuja,” alisema Julie Mbuyi, mama wa watoto wawili mwenye umri wa miaka 45, ambaye alikuwa amevalia mavazi yaliyokuwa na ujumbe wa Papa Francis.

“Alifurahi sana kumuona na usiku ule kabla ya kuwasili kwa papa hakuweza kulala!”

Umati wa watu ulishangilia tena wakati Papa huyo mwenye asili ya Argentina alipowasalimia kwa lugha ya Kilingala, moja wapo ya lugha nne za kitaifa za Congo ambayo inazungumzwa na watu wengi katika mji mkuu wa Kinshasa.

Vilevile, walisikiliza kwa makini alipokuwa akihubiri akiwasihi Wacongo kufungua mioyo yao ili wasamehe, alitoa mfano wa Yesu ambaye aliwasamehe wale waliomsaliti.

“Aliwaonyesha majeraha yake, kwa sababu msamaha huzaliwa kutokana na majeraha,” Francis alisema.

“Unazaliwa wakati majeraha yetu hayaachi makovu ya chuki, bali yanakuwa njia yakuwapa wengine nafasi na kukubali udhaifu wao.Udhaifu wetu unakuwa fursa, na msamaha unakuwa njia ya amani.”

Kadhalika, akielezea miongo kadhaa ya ghasia hasa Mashariki mwa Congo ambako imewalazimu mamilioni kukimbia makazi yao, Francis alisisitiza kusamehe hakumaanishi kujifanya kuwa hakuna kitu kibaya kilichotokea.

Fauka ya hayo, lakini alisema kitendo cha msamaha kinajenga “kuuacha moyo huru.”

  • Tags

You can share this post!

Uhuru aonja kiboko cha Ruto

Ishara wandani wa Murungi kujiunga na serikali ya Mwangaza

T L