• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 11:15 AM
DINI: Unahitaji hekima kucheza karata zako vyema maishani na usikubali hofu ikuwekee vikwazo

DINI: Unahitaji hekima kucheza karata zako vyema maishani na usikubali hofu ikuwekee vikwazo

FAUSTIN KAMUGISHA

 

KULINGANA na Edward de Bono, kuwekeza ni suala la namna unavyocheza karata ulizopewa.

Mwalimu aliwaeleza wanafunzi wake kwamba atawauliza swali na na atampa simu atakayelijibu.

Lakini pia akasema kuwa, mwanafunzi ambaye angemuuliza swali na yeye ashinde, basi atamrudishia simu yake.

“Yesu alilisha wanaume wangapi chakula?” aliuliza.

Naye mwanafunzi alijibu kuwa walikuwa 5,000.

Alipewa simu. Naye mwanafunzi alimuliza mwalimu alimtaka mwalimu kutaja majina ya watu hao, jambo ambalo hakuweza na akapoteza simu hiyo. Kutokana na hali hii, basi tunasema kuwa ilikula kwake.

Mwalimu hakucheza vizuri karata zake.Katika Biblia kuna masimulizi juu ya watu watatu waliopewa talanta na bwana wao aliyesafiri. Aliyepewa talanta tano alitengeneza faida nyingine tano.

Aliyepewa talanta mbili alitengeneza faida ya talanta mbili. Aliyepewa talanta moja aliizika.

Alimwambia bwana wake, “basi nikaogopa, nikaenda nikaficha talanta yako katika ardhi” (Mt. 25 : 25).

Aliyepewa talanta moja hakushughulika, ilikula kwake. Jitahidi katika maisha isile kwako. Ukiogopa kuwekeza inakula kwako.

“Ole wao ambao hawaimbi kamwe, lakini wanaaga dunia muziki wao wote ukiwa ndani mwao,” alisema Oliva W Holmes.

Kuna hatua saba za kushindwa kifedha. Kinyume chake ni hatua saba za kushinda kifedha.

Kwanza ni kuwa na hofu. Kuwa na hofu ni hatua ya kwanza ya kushindwa. Kuwa na ujasiri ni hatua ya kwanza ya kushinda. Fikiria una ndugu ambaye amezaliwa bila mkono wa kulia na nusu ya mguu wa kulia. Fikiria akiwa na umri wa miaka sita anakuuliza, “Unafikiri nitaweza kushiriki michezo shuleni? Utamwambia nini? Au utamweleza hali halisi?’ Fikiria siku moja mnatazama mechi kwenye runinga naye anakuuliza, “Unafikiri nitawahi siku moja kucheza mpira?’ Utamwambia nini? Fikiria, siku moja anakuona unafungua kurasa kwenye kitabu cha rekodi cha ligi za mpira. Anakuuliza, siku moja nitacheza mpira vizuri na jina langu kuingizwa kwenye kitabu hicho? Utamwambia nini?

Mwaka 1953, mtoto mwenye umri wa miaka sita aitwaye Tom Dempsey alikuwa anauliza maswali kama haya kama ndugu yako wa kufikirika naye alizaliwa bila mkono wa kulia na nusu ya mguu wa kulia.

Tom alienda shule na kucheza mpira wa Marekani. Alicheza timu ya Junior College California. Badaye alisajiliwa kwenye timu ya New Orleans Saints.

Novemba 8 1970, timu ya Saints ilikuwa imechapwa 17 kwa 16 na Detroit. Zilibaki sekunde mbili mchezo kumalizika. Kocha J. D Roberts alimgusa Tom na kumwambia, “Ipe timu yako shuti nzuri sana.” Tom alitoa shuti nzuri sana na timu yake ilishinda kwa 19 – 17.

Alitumia kipaji kimoja alichokuwa nacho kufanya maajabu. Tom hakuwa na hofu na hali aliyokuwa nayo.

Aliyepewa talanta moja alisema, “niliogopa’ (Mt. 25: 25).

“Kila kitu unachohitaji kipo upande mwingine wa hofu.”

Jack Confield aliwahi kusema. Ilipo hofu yako ndipo yalipo mafanikio yako. Unaogopa kupeleka ndizi Ulaya, huko ndipo yalipo mafanikio yako. Unaogopa kumiliki duka, huko ndiko yapo mafanikio yako. Kulingana na Gandhi, “Adui ni hofu. Tunafikiri ni chuki kumbe ni hofu.” Ili kuvumbua bahari mpya lazima uende mbali lazima ufanye kitu. “Mtu ambaye hajiweki katika hali ya hatari, hafanyi lolote, hana chochote, na si chochote na atakuwa si chochote. Anaweza kukwepa mateso na huzuni, lakini hawezi kujifunza kuishi na kubadilika na kukua na kupenda na kuishi,” alisema Leo F. Buscaglia (1924 – 1998)Marekani anayetambulika kwa kuhimiza kuhusu upendo.Kama kila mtu angejitahidi kufanya lolote zuri duniani ingekuwa mahali pazuri pa kukalika (Itaendelea wiki ijayo).

You can share this post!

CBC: Sossion awasilisha malalamiko ya wazazi bungeni

TAHARIRI: Ripoti ya Kemsa inakatisha tamaa