• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 6:50 AM
FAO yahimiza vijana wawe mstari wa mbele katika shughuli za kilimo

FAO yahimiza vijana wawe mstari wa mbele katika shughuli za kilimo

Na SAMMY WAWERU

SHIRIKA la Chakula na Kilimo (FAO-UN) limewahimiza vijana kukumbatia shughuli za kilimo-biashara ili kuongeza kiwango cha uzalishaji wa chakula.

Mkurugenzi Mkuu wa FAO, Dkt Qu Dongyu amesema changamoto zinazozingira sekta ya kilimo zitaangaziwa ipasavyo endapo nguvu mpya itajumuishwa katika mtandao wa uzalishaji chakula.

Alisema hayo wakati akizungumza kupitia kikao cha mtandao, kufuatia kongamano la Kimataifa la Chakula linaloendelea na lililoanza Ijumaa, Oktoba 1.

Dkt Qongyu alisema maendeleo katika sekta ya kilimo yatashuhudiwa kwa kuzindua mikakati tofauti, ikiwemo kushirikisha vijana katika shughuli za kilimo na ufugaji.

Aidha, alieleza haja ya kuwa na ubunifu ili kuboresha sekta ya kilimo na uzalishaji wa chakula, kila familia ulimwenguni iwe na maisha bora.

“Athari za janga la Covid-19, mabadiliko ya tabianchi, wadudu na magonjwa zimechangia uhaba wa chakula unaotukumba. Tunapaswa kutathmini masuala kwa kina.

“Kwa kujumuisha nguvu mpya, vijana watasaidia kuleta mabadiliko makubwa,” Dkt Dongyu akafafanua, akisema mkondo huo utasaidia kuimarisha mambo.

Huku vijana wengi ulimwenguni wakilalamikia kutohusishwa katika maamuzi ya maendeleo ya nchi wanazotoka na pia katika uongozi, Mkurugenzi Mkuu huyo alisema haja ipo kuwapiga jeki, akitaja mchango na ubunifu wao hasa katika masuala teknolojia na kidijitali kama vigezo na nguzo muhimu kuboresha sekta ya kilimo na uzalishaji wa chakula.

“Vijana ndio matumaini ya siku zijazo. Wana mtazamo wa kuleta maendeleo,” Dkt Dongyu akasisitiza.

Kikao hicho kilichopeperushwa kupitia mtandao wa Zoom pia kilihudhuriwa na wadauhusika, akiwemo Bi Fabiana Dadone ambaye ni Waziri wa Masuala na Mikakati ya Vijana Italia.

Bi Dadone alieleza Imani yake kwa vijana kusaidia kulinda mazingira na kuangazia mabadiliko ya tabianchi.

Kongamano la Chakula Duniani (World Food Forum) linaloendelea na la kwanza kushirikisha vijana, pia linatumia sanaa kufanya hamasisho na kutoa mchango na ubunifu kuboresha sekta ya kilimo.

Limeandaliwa Rome, Italia na linaendelea hadi Oktoba 5, 2021.

Kenya ni miongoni mwa mataifa ambayo yameibuka na mikakati maalum kushirikisha vijana katika sekta ya kilimo, ili kuongeza kiwango cha uzalishaji wa chakula.

“FAO – Kenya tunatambua mchango wa vijana katika kilimo. Tumezindua miradi mbalimbali kwa ushirikiano na serikali, na kuwapa vijana motisha kushiriki na kuendeleza shughuli za kilimo.

“Hatua ya Rais Uhuru Kenyatta kufufua mpango wa 4K Club shuleni ni afueni kwa taifa ili kukuza na kushirikisha vijana katika sekta ya kilimo. Utasaidia kuiboresha na kuongeza chakula,” akasema Hamisi Williams, Naibu Mwakilishi FAO-Kenya.

Juni 2021, Rais Kenyatta alifufua mpango wa 4K Club, kuanza kutekelezwa katika shule zote za msingi na upili nchini.

Mwezi Julai, Waziri wa Kilimo, Bw Peter Munya aliongoza hafla ambapo shule 10 katika Kaunti ya Nairobi zilipokea miche 10, 000 ya mboga kutoka kwa Ubalozi wa Israili hapa Kenya.

You can share this post!

Rennes wapiga PSG breki kali katika kampeni za Ligue 1

Liverpool, Manchester City nguvu sawa ligini