Na WANDERI KAMAU
JE, ni nani “mkarimu” kati ya kiongozi wa ODM, Bw Raila Odinga, na Naibu Rais William Ruto?
Hilo ndilo swali lililozua gumzo wiki hii, baada ya Dkt Ruto kumlaumu Bw Odinga kwa kuwa mkono gamu kwa wafuasi wake, licha ya kuendelea kumuunga mkono kwa muda mrefu.
Baada ya kauli hiyo, Dkt Ruto alijipata pabaya, baada ya bintiye Bw Odinga, Bi Winnie Odinga, kumkabili vikali, akisema si lazima Bw Odinga aweke michango yake hadharani.
Kando na Winne, washirika wengine wa Bw Odinga walijitokeza kukosoa kauli ya Dkt Ruto.
Dkt Ruto alitoa kauli hiyo alipokutana na ujumbe kutoka Kaunti ya Kajiado, uliomtembelea katika makazi yake, mtaani Karen, jijini Nairobi.
Naibu Rais William Ruto: “Rafiki yangu (Raila) ambaye tunashindana naye huwa hahudhurii michango ya pesa katika shule, makanisani au katika vikundi ya akina mama. Hata kutoa sadaka kanisani ni tatizo kwake. Baadhi ya watu wana bahati sana kwani huwa wanapata kura kutoka kwa watu ambao hawajawafanyia chochote kwa muda mrefu.”
Winnie Odinga, mwanawe Raila: “Si michango yote inayopaswa kutangazwa hadharani. Unapaswa kutoa kwa roho yako yote au kutotoa kabisa. Si lazima dunia yote ijue. Hayo ndiyo mafundisho ya vitabu vitakatifu.”