Na THOMAS MATIKO
KWA wasanii wengi kama sio muziki, wangekuwa wakifanya kazi nyingine za kitaaluma zaidi.
Kwa mfano Nameless ni mchora ramani, yule Maureen Kunga wa bendi ya Elani kasomea Uwakili na Avril akiwa ni mtaalamu wa usanifu mijengo (interior design). Wengine wengi pia wana taaluma za dizaini hizo.
Ila kwa rapa wa gengetone Mejja, mambo yake ni tofauti kidogo.
Utashangaa kusikia kuwa, kama sio muziki angekuwa ni dereva wa malori.
“Dhamira yangu haipendi kabisa kazi ya kukaa sehemu moja. Kwamba kila leo naripoti kwenye stesheni fulani. Kama sio muziki nafikiri ningeishia kuwa dereva wa trela sababu napenda sana safari,” Mejja kafunguka.
Kwa bahati, nzuri muziki wake umekuwa ukipokelewa vizuri nchini na kumfanya kuwa mmoja kati ya wasanii wakubwa wasiokosa shoo za kulipwa nchini.