• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 10:50 AM
KAULI YA MATUNDURA: Shabaan Robert na Muyaka walinyanyasa na kudhulumu wanawake katika tungo zao?

KAULI YA MATUNDURA: Shabaan Robert na Muyaka walinyanyasa na kudhulumu wanawake katika tungo zao?

Na BITUGI MATUNDURA

NILIPOHUDHURIA Maonesho ya Kimataifa ya Vitabu ya Kila mwaka jijini Nairobi mnamo 2018, nilizuru ‘kibanda’ cha Taasisi ya Taaluma ya Kiswahili (TATAKI) kujionea machapisho mapya katika fasihi na Isimu ya Kiswahili.

Maonesho hayo huandaliwa kila mwaka na Chama cha Wachapishaji wa Vitabu cha Kenya (KPA). Mojawapo ya vitabu nilivyovinunua ni Chanjo, Matakwa ya Mwanamume Katika Mwili wa Mwanamke (Muhammed Seif Khatib, 2014). Ingawa kitabu hiki kilichapishwa takriban miaka sita iliyopita, sikupata fursa ya kukisoma kwa sababu sikuwa nimehudhuria maonesho hayo kwa kipindi cha miaka minne. Muhammed Seif Khatib ni mwandishi, mhakiki na vilevile mwanasiasa.

Kazi yake maarufu katika ulingo wa fasihi ni diwani yake ya Wasakatonge (OUP,2003). M.S. Khatib ni mhakiki ambaye misimamo yake katika uhakiki wa fasihi ya Kiswahili imewahi kuzua midahalo miongoni mwa wasomi wa fani hizo. Kwa mfano, msimamo wake katika mdahalo kuhusu Utendi wa Mwanakupona (1850) ni kwamba: “Utendi wa Mwanakupona ni ‘sumu’ inayolenga kuhalalisha dhuluma na ukandamizwaji wa mwanamke katika asasi za jamii.”

Mwengo wa msimamo huu unajitokeza tena katika kitabu chake ambacho nimekwisha kukitaja. Katika kitabu hiki, Khatib anachunguza kwa kina na kufanya uhakiki wa kiulinganifu baina ya washairi wawili mahashumu katika fasihi ya Kiswahili – Muyaka bin Haji na Shaaban bin Robert. Baadhi ya maswali ambayo amejikusuru kuyatalii katika kitabu hiki ni pamoja na: Ni vipi Muyaka bin Haji na Shaaban bin Robert ambao waliishi katika jamii na nyakati tofauti wanafanana na wakati huohuo kutofautiana katika mitazamo na matakwa yao kuhusu taswira ya mwanamke?

Je, zipo athari za kisiasa, kidini, kielimu na kiuchumi kuhusu mitazamo yao kumhusu mwanamke? Mwisho, kitabu chake kimelenga kuchochea mwamko wa ukombozi wa fikra juu ya mwanamke kwa misingi kwamba wanawake ni kundi la kutengwa na kunyanyaswa kwa kipindi kirefu mno – hususani katika asasi za jamii.

Je, Muyaka bin Hajji na Shaaban bin Robert walishiriki na au kuchangia vipi katika ‘ujambazi’ wa kumkandamiza na kumdhalilisha mwanamke katika mashairi yao? Walifanya hivyo kwa kujua au kutojua? Vipi?

Katika kitabu chake, M.S.Khatib anadai kwamba dhamira ya Muyaka bin Haji ya kebehi na dharau inamlenga mwanamke ambaye anakataa udhibiti. Jazanda alizozitumia Muyaka katika tungo zake chambacho Khatib, zinamweka mwanamke katika nafasi ya unyonge na kulazimika kurudi kwa mwanamume kwa shingo upande na kuwa udhibiri wake. Naye Shabaan bin Robert – licha ya kumsifu mwanamke kwa kumumithilisha na ‘ua’ katika mashairi yake mengi kuusifia urembo wake, wakati mwingine anamgeuka (mwanamke huyo) na kumwita ‘malaya’ kwa majina ya kebehi kama vile ‘magune’, ‘pangapunge’, ‘makuyembesa’ na ‘vigwene’.

Kitabu cha Khatib kinachangia upya mdahalo kuhusu suala la taswira ya mwanamke katika fasihi ya Kiswahili. Kwa bahati mbaya, Mohamed Seif Khatib alifariki mapema mwaka huu. Hata hivyo, tunaliwazika na kufarijika kwamba ‘waandishi hawafi’. Huendelea kuishi katika tungo na maandishi yao. Hii ndiyo sababu tungali tunamkumbuka William Shakespeare wa Uingereza – hata ingawa alifariki takriban miaka 400 iliyopita.

You can share this post!

Kocha Ryan Mason aaminiwa nafasi ya kushikilia mikoba ya...

Kila kaunti kupata daktari wa mifugo atakayesaidia kuondoa...