NA MARGARET MAINA
Vyakula vya wanga nyingi
Kula chakula chenye wanga kinaweza kudhoofisha afya kwa muda mrefu kwani husababisha kuongezeka kwa uvimbe na kubadilisha utumbo. Kwa mfano, viazi vinaweza kuchukuliwa kuwa chakula chenye wanga lakini wali, pasta, au donati ni hatari zaidi kwa mwili kwani zina wanga iliyopitiliza.
Chakula cha kukaanga
Chakula cha kukaanga hakifai kwani hudhuru mwili katika viwango mbalimbali. Sio tu kinaongeza pauni kwenye mwili lakini pia ni kigumu kusagika. Kwa kuwa mwili huona ugumu wa kumeng’enya, chakula hicho kinaweza kusababisha kuhara au uvimbe. Kiwango cha nyuzinyuzi katika vyakula vingi vya kukaanga ni kidogo na hivyo huvifanya kuwa vigumu kusagika.
Chakula cha viungo vingi
Viungo huongezwa kwa chakula ili kuchochea mfumo wa utumbo. Lakini kwa watu wengine, viungo vingi huwa na athari mbaya. Watu wengi hupata gesi, uvimbe, kiungulia, asidi na hata maumivu ya tumbo kwa kula chakula chenye viungo vingi. Vyakula vyenye viungo vinapaswa kuepukwa haswa unapokaribia wakati wa kulala.
Vyakula vyenye nyuzinyuzi nyingi
Chakula chenye nyuzinyuzi nyingi kinaweza kuwa kigumu kusagika kwani tumbo linahitaji juhudi zaidi kukivunja. Chakula chenye nyuzinyuzi nyingi ni pamoja na mboga mbichi, dengu, maharagwe na wali wa kahawia. Hata mboga huingia kwenye orodha inayofahamika kama ‘orodha mbaya zaidi ya vyakula kwa afya ya usagaji chakula’. Ndiyo, mboga mbichi ni nzuri kwa afya yako, lakini muhimu ni kiasi. Kwa kuwa mboga mbichi zina nyuzinyuzi nyingi, aina zisizoyeyuka zinaweza kusababisha gesi, uvimbe, kuhara na matatizo mengine kama hayo ya tumbo.
Pombe
Pombe ni mbaya kwa tumbo na ini. Ni sumu kwa mwili na husababisha shida kali za kiafya kama ugonjwa wa cirrhosis na ulevi.
Hata kiasi cha wastani cha pombe kinaweza kulegeza umio na kusababisha kiungulia na asidi. Kwa kiasi kikubwa, pombe inaweza kusababisha kuvimba kwa utando wa tumbo, tumbo na kuhara. Zaidi ya hayo, pombe ina kalori tupu tu na inapunguza kasi ya michakato ya kimetaboliki ya mafuta katika mwili.
Bidhaa za maziwa
Maziwa na bidhaa za maziwa ni ngumu kusagika kwa kila mtu japo hali hii ni zaidi kwa baadhi ya watu kuliko kwa wengine. Hii ni kutokana na uwepo wa lactose – aina ya sukari inayopatikana katika bidhaa za maziwa. Wakati mfumo wa tumbo ya mtu hauwezi kusaga kundi hili la chakula, hupata gesi, uvimbe na wakati mwingine kichefuchefu. Ulaji wa bidhaa nyingi za maziwa unaweza kusababisha ugonjwa wa kuhara unapoingia kwenye utumbo.