• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 1:20 PM
WANTO WARUI: Huenda wanafunzi wengi wakakosa mitihani ya KNEC

WANTO WARUI: Huenda wanafunzi wengi wakakosa mitihani ya KNEC

Na WANTO WARUI

Baraza la mitihani nchini (KNEC) linapanga kuwapa wanafunzi wa Gredi ya 1-3 na madarasa ya 5-7 majaribio ya kutathmini kiwango chao cha uelewa kuanzia Jumatatu hadi Ijumaa, 22-01-2021.

Hii ni kutokana na hali iliyowakumba wanafunzi ya kukaa nyumbani kwa kipindi cha miezi tisa kutokana na mkurupuko wa ugonjwa wa Covid-19.

Kwa mujibu wa KNEC, wanafunzi wote wanatarajiwa kuwa shuleni ili waweze kufanya majaribio hayo ambayo tayari yameandaliwa na KNEC na kutumwa shuleni kupitia njia ya mtandao.

Hivi ni kusema kuwa KNEC inatarajia kila shule nchini iwe na uwezo wa kupata majaribio hayo, iweze kusimamimia wanafunzi wafanye kisha isahihishe kazi hiyo na kutuma majibu yaliyotolewa na wanafunzi kwake (KNEC) kupitia njia iyo hiyo ya mtandao. Hali ilivyo sasa, kuna wanafunzi wengi ambao bado hawajarudi shuleni na hali zao za kuendelea na masomo hazijulikani.

Miongoni mwao ni wasichana ambao walipata mimba, wengi wao sasa wakiwa katika hatua za mwisho za kupata watoto. Kwao itakuwa vigumu mno kuweza kufikia majaribio haya.

Shuleni nako changamoto ni nyingi. Wanafunzi waliorudi shuleni bado hawana madawati ya kutosha. Wengine wanasomea chini ya miti kulikojaa upepo na mavumbi.

Shule nyingi nchini hazina umeme wala kompyuta. Haitakuwa jambo rahisi kwa walimu kuweza kusimamia mitihani hii katika hali kama hizi.Kuna baadhi ya shule ambazo zilifungwa kutokana na mafuriko ya maziwa kama vile Baringo, Nakuru na Naivasha.

Sehemu kubwa ya wanafunzi hao huenda bado iko nyumbani kutokana na hali ya umaskini ya wazazi. Ni wazi kuwa wanafunzi kama hawa hawatapata fursa ya kufanya majaribio haya.

Wati ambapo wanafunzi wa kidato cha nne, darasa la nane na gredi ya nne walipokuwa shuleni, KNEC iliweza kuandaa majaribio kama haya. Ingawaje shule zilijizatiti kusimamia, kuna shule nyingine ambazo hazikutoana matokeo sahihi.

Kufikia sasa, KNEC bado haijaweza kutoa matokeo ya tathmini la Gredi ya 4 kwa walimu.Hivi ni kusema kuwa, majaribio yanayotarajiwa kuanza leo yatakuwa na changamoto kwa walimu na wanafunzi wenyewe.

Kuna wale ambao wataweza tu kufanya nusu ya majaribio hayo huku wengine wakishindwa kabisa. Ijapokuwa KNEC inafanyiza zoezi hili ikiwa na nia nia ya kutathmini kiwango cha uelewa wa wanafunzi tu, itakuwa si vyema kuwakosesha wanafunzi wengi kiasi hiki kushiriki zoezi kama hili.

Mpango huu wa KNEC wa kutathmini wanafunzi kwa njia hii ungefaulu zaidi endapo serikali kufikia sasa ingekuwa ishatekeleza ahadi yake ya awali ya kupeana kompyuta kwa wanafunzi. Hali ilivyo sasa, itabidi wanafunzi wengi waikose mitihani hii.

You can share this post!

Ruto na Raila hawafai kupuuza agizo la Rais

MARY WANGARI: Kenya na Somalia zitafute njia ya kutatua...