• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 1:20 PM
WARUI: Tukumbatie changamoto za CBC ili utekelezaji uwe rahisi

WARUI: Tukumbatie changamoto za CBC ili utekelezaji uwe rahisi

Na WANTO WARUI

MFUMO mpya wa Elimu (CBC) ambao kwa sasa umefika Gredi ya 5 bado haujapokelewa vyema na asilimia kubwa ya Wakenya.

Akisisitiza kuwa mfumo huu utaendelea kote nchini, Waziri wa Elimu Profesa George Magoha, juma lililopita alisema kuwa ni makosa kuulaumu mfumo wenyewe kwa kusema kuwa ni ghali mno ilhali vifaa vingi ambavyo vinaweza kutumiwa kufanikisha masomo vinapatikana katika mazingira yetu tena kwa urahisi.

Waziri Magoha aliwaambia wazazi wanaolalamikia gharama ya elimu ya CBC kuwa serikali inatoa vitabu vya kiada katika kila shule ya umma pamoja na kuhakikisha kuwa walimu wamepata mafunzo ya mara kwa mara ili kuwawezesha wasaidie wanafunzi.

Waziri alisema kuwa changamoto ambazo wazazi na walimu wanakumbana nazo ni zile tu za kawaida ambazo ni lazima ziwepo wakati jambo jipya linaanzishwa.

Mfumo mpya wa CBC ulianzishwa baada ya majopo kadhaa kuwasilisha mapendekezo yake kwa serikali ili kubadilisha mfumo uliopo wa 8-4-4 ambao unaegemea mitihani zaidi kuliko kutoa elimu ya kumwezesha mwanafunzi kujitegemea.

Kidesturi, mfumo wowote wa elimu unahitaji kuambatana vyema na mahitaji ya jamii. Kuna mambo mengi ambayo hubadilika kadri miaka inavyosonga na ni sharti elimu pia ibadilike ili kukidhisha mahitaji ya watu.

Mfumo wa 8-4-4 umekuwako nchini kwa muda wa miaka 36 tangu 1985. Mambo mengi yamebadilika tangu kuanzishwa kwake hasa ya kiteknolojia na jinsi ya kutenda kazi.

Aidha, watoto wanaozaliwa sasa ni wa kizazi kingine tofauti kabisa kwa hivyo kuwapa wanafunzi hawa elimu isiyoambatana na mahitaji yao ya kimaisha ni kuwakosea na kutojali maisha yao ya baadaye.

Lengo

Lengo No. 4 katika Malengo ya Kitaifa ya Elimu huwa linaelezea kuwa elimu inastahili kuandaa raia mwadilifu na mwenye misingi bora ya kidini kama ilivyoelezwa katika Katiba ya Kenya.

Hii ndiyo sababu mfumo wa CBC umeteuliwa ili uweze kuwiana na mahitaji haya.Kwa minatarafu hii, kuna haja Wakenya wote kuelewa sababu za kuanzishwa kwa mfumo huu, tuuelewe mfumo wenyewe na tuelewe mahitaji ya watoto wa taifa hili kabla ya kukashifu masomo yake.

Kwa sasa kila kitu duniani kinaelekea kutekelezwa kidijitali; njia ambayo elimu ya CBC inasisitiza itumiwe katika masomo shuleni. Japo mfumo wenyewe unaonekana kuwa ghali au mgumu, wanafunzi ambao wako shuleni na wanaofunzwa masomo ya CBC inavyostahili wanafurahia masomo haya zaidi ikilinganishwa na mfumo unaoondoka.

Tunapotatizika kutokana na mambo kadhaa yaliyomo katika CBC, hatuna budi tuelewe kuwa hata jambo lolote jepesi vipi huonekana kuwa gumu linapoanzishwa.

You can share this post!

STEPHEN JACKSON: Mifumo thabiti ya lishe kufaa uchumi na...

Kilio cha Wakenya waliobamizwa ukutani na bei ya juu ya...