MNAMO Jumamosi Naibu Rais William Ruto aliahidi kuanzisha miradi kadhaa ya uzalishaji chakula kupitia kilimo cha unyunyiziaji katika Kaunti ya Turkana akishinda urais Agosti 9.
Akiendesha kampeni katika maeneo mbalimbali kaunti hiyo, Dkt Ruto, alisema serikali yake itakomesha kabisa kero ya baa la njaa ambalo huzonga wakazi wa kaunti hiyo kila mara.
Lakini, asije akasahau kuwa mnamo Julai 10, 2017, yeye na Rais Uhuru Kenyatta, waliahidi kuchimba visima katika eneo la Lokitipi lililoko eneo bunge la Turkana Mashariki kuwezesha kupatikana kwa maji ya matumizi nyumbani, kilimo na mifugo. Eneo hilo limebainika kuwa na maji mengi chini ya ardhi.
Lakini miaka mitano baadaye, ahadi hiyo haijatimizwa, na Jumamosi Dkt Ruto, hakutoa sababu ya kutotekelezwa kwa mradi huo. Aliendelea kutoa ahadi sawa na zile alizotoa 2017.