• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 4:55 PM
Auka Gecheo ataka Kenya kufanya zaidi kufikia Uganda kwenye soka

Auka Gecheo ataka Kenya kufanya zaidi kufikia Uganda kwenye soka

Na GEOFFREY ANENE

AUKA Gacheo ametoa changamoto kwa Kenya na wanachama wengine wa Baraza la Mashirikisho ya Soka ya Afrika Mashariki na Kati (CECAFA) kutumia fursa ya Uganda kufika fainali ya Kombe la Afrika Under-20 kama kichocheo cha kuimarisha soka yao.

Mkurugenzi huyo mkuu wa Cecafa, ambaye alijaza nafasi ya Mkenya mwenzake Nicholas Musonye kwenye baraza hilo mwezi Machi 2020, alisifu Uganda Hippos kwa kung’ara katika mashindano hayo ya mataifa 12.

Hippos, ambao walikuwa wakishiriki dimba hilo kwa mara ya kwanza kabisa, walipoteza 2-0 dhidi ya Black Satellites ya Ghana mnamo Machi 6 nchini Mauritania.

“Kama eneo la Cecafa, tunafurahia sana kuwa tulikuwa na timu katika fainali ya Afcon U-20. Ni ishara ya bidii na kujitolea kwa Shirikisho la Soka Uganda (FUFA) katika kuimarisha soka yake mashinani na ya chipukizi,” Auka alieleza tovuti ya baraza hilo mnamo Machi 8.

“Tunajivunia sana jinsi Uganda ilinadi eneo letu vyema kwenye kombe hilo,” aliongeza.

Chini ya kocha Morley Byekwaso, Hippos ilishinda michuano minne kati ya sita ambayo ilisakata katika makala hayo ya 16. Ilianza kampeni yake kwa kuchabanga Msumbiji 2-0 kabla ya kupoteza dhidi ya Cameroon na kukamilisha Kundi A kwa kunyamazisha wenyeji Mauritania 2-1.

Ushindi dhidi ya Msumbiji na Mauritania ulitosha kuwapa Waganda tiketi ya robo-fainali ambapo walibandua Burkina Faso kwa njia ya penalti 5-3 baada ya dakika 120 kutamatika 0-0.

Walikung’uta Tunisia 4-1 katika nusu-fainali kabla ya kuzidiwa maarifa na Ghana ambayo ilitwaa taji lake la nne.

Uganda ilinyakua mataji ya kocha bora kupitia Byekwaso, mfungaji bora Derrick Kakooza aliyechana nyavu mara tano na pia Hippos kuwa timu hiyo iliyoonyesha nidhamu ya hali ya juu.

Serengeti Boys ya Tanzania pia iliwakilisha eneo la Cecafa, ingawa haikufanya vyema. Ilitoka 1-1 dhidi ya Gambia kabla ya kupoteza dhidi ya Ghana 4-0 na Morocco 3-0 katika Kundi C na kuaga mashindano.

You can share this post!

Dalili Klopp yuko karibu kuagana na Liverpool

Watambue wanawake bomba walio chini ya miaka 30