• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 6:55 AM
Awiti ashinda gofu ya Safaricom mjini Eldoret kuingia fainali kubwa

Awiti ashinda gofu ya Safaricom mjini Eldoret kuingia fainali kubwa

Na GEOFFREY ANENE

ALICE Awiti kutoka Nyanza aliibuka mshindi wa duru ya sita ya mashindano ya gofu ya Safaricom Golf Tour baada ya kuzoa alama 49 katika shindano la kusisimua katika klabu ya gofu ya Eldoret.

Afisa huyo kutoka kampuni ya Safaricom alizoa pointi 23 katika mashimo tisa ya kwanza na pointi 26 katika mashimo tisa ya mwisho kuwa na jumla ya pointi 49.

Yeye ni mshindi wa sita katika mashindano hayo ya duru 14. Ushindi wake ulimtunuku tiketi ya kuwania taji katika fainali kubwa katika klabu ya gofu ya Vipingo Ridge mwezi Agosti.

Awiti anaungana na washindi wa duru tano za kwanza Cyprian Bundi (Nanyuki), mwanagofu chipukizi Leo Gitonga (Limuru), Zain Manji (Muthaiga), Lydia Jebichii (Nyanza) na Simon Kimatu (Machakos) katika fainali uwanjani Vipingo Ridge.

“Ushindi hapa Eldoret umenishtua kwa sababu sikuutarajia kabisa katika taaluma yangu ya gofu. Ni mara ya kwanza kabisa mimi kushinda shindano lolote na inanifanya nijivunie kazi yangu na kuongeza bidii ili nipate mafanikio zaidi. Ingawa matokeo yangu yamekuwa mazuri, nilipata changamoto kadhaa katika kutumbukiza mpira shimoni. Nitashughulikia idara hiyo ya mchezo wangu ninapojiandaa kwa fainali kubwa,” alisema Awiti.

Duru ya Eldoret ilivutia wanagofu 140 kutoka maeneo ya Bonde la Ufa pamoja na viunga vyake zikiwemo kaunti za Kisumu, Bungoma, Kakamega na Trans Nzoia. Duru ijayo itaandaliwa uwanjani Karen jijini Nairobi mnamo Mei 13.

  • Tags

You can share this post!

Kundi lapendekeza Ruto ateue Waiguru kuwa naibu wake

Kibaki asifiwa kama aliyeenzi bidii ya maafisa

T L