Na MASHIRIKA
BRAZIL imekuwa timu ya kwanza kutoka Amerika Kusini kufuzu kwa fainali zijazo za Kombe la Dunia za 2022 nchini Qatar baada ya kusajili ushindi wa 1-0 dhidi ya Colombia katika uwanja wao wa nyumbani.
Lucas Paqueta, 24, alikuwa mfungaji wa bao la pekee na la ushindi katika mchuano huo uliotandaziwa ugani Neo Quimica Arena jijini Sao Paulo. Kiungo huyo wa Olympique Lyon nchini Ufaransa alishirikiana vilivyo na wanasoka wawili wa Paris Saint-Germain (PSG) – Marquinhos na Neymar.
Brazil ambao ni mabingwa mara tano wa Kombe la Dunia wangali na michuano sita zaidi za kusakata katika safari ya mechi za vikosi vya Amerika Kusini kuelekea Qatar. Kufikia sasa, masogora hao wa kocha Adenor ‘Tite’ Bacchi wamepoteza alama mbili pekee kutokana na mechi 12 zilizopita na pengo la pointi tisa linatamalaki kati yao na nambari mbili Argentina.
Mechi ijayo itakayosakatwa na Brazil ni gozi la ugenini litakalowakutanisha na washikilizi wa taji la Copa Amerika, Argentina, katika mji wa San Juan mnamo Novemba 16, 2021.