• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 7:02 PM
Brighton waangusha Man-Utd ya kocha Ten Hag katika EPL ugani Old Trafford

Brighton waangusha Man-Utd ya kocha Ten Hag katika EPL ugani Old Trafford

Na MASHIRIKA

BRIGHTON walimkaribisha kocha Erik ten Hag wa Manchester United kwenye Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) hapo jana kwa kichapo cha 2-1 uwanjani Old Trafford.

Sajili wapya wa Man-United – Christian Eriksen na Lisandro Martinez – walipangwa katika kikosi cha kwanza huku Cristiano Ronaldo aliyeibuka mfungaji bora wa mabingwa hao mara 20 wa EPL muhula jana kwa mabao 18 akiletwa ugani katika kipindi cha pili kujaza nafasi ya Fred.

Pascal Gross alipachika wavuni mabao yote mawili ya Brighton katika kipindi cha kwanza kabla ya masogora wa Ten Hag kufutiwa machozi na Alexis Mac Allister aliyejifunga katika dakika ya 68.

Ushindi wa Brighton uliendeleza ubabe wao dhidi ya Man-United waliopokea kichapo cha 4-0 kutoka kwa kikosi hicho cha mkufunzi Graham Potter mnamo Mei ugani Amex. Ulikuwa pia ushindi wa kihistoria kwa Brighton walioshuka dimbani wakiwa wamepoteza mara nane na kuambulia sare moja kutokana na mechi tisa za awali dhidi ya Man-United ugenini.

Matokeo ya jana ya Man-United yalirejesha kumbukumbu za 2014 ambapo kocha wao wa zamani, Louis van Gaal, alikaribishwa pia EPL kwa kichapo cha 2-1 kutoka kwa Swansea City ugani Old Trafford.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

  • Tags

You can share this post!

Borussia Dortmund wakomoa Leverkusen katika Bundesliga

Jinsi vijana, wanamuziki walivyopiga kampeni za Azimio eneo...

T L