Na GEOFFREY ANENE
HARAMBEE Stars imeingia kambini Machi 11 kujiandaa kwa mechi ya kupimana nguvu dhidi ya majirani Sudan Kusini itakayosakatwa ugani Nyayo mnamo Machi 13.
Sudan Kusini anayochezea mshambuliaji wa Gor Mahia Tito Okelo, iliwasili nchini Jumanne na tayari imekuwa na vipindi kadhaa vya mazoezi.
Wachezaji wote wanaocheza katika Ligi ya nyumbani isipokuwa Samuel Olwande, Bonface Onyango, Daniel Sakari, James Mazembe na Erick Kapaito kutoka klabu ya Kariobangi walifika kambini.
Waliokosa mazoezi walifanya hivyo kwa sababu ya kuwa na majukumu ya Ligi Kuu.
Baada ya kuvaana na Sudan Kusini hapo Jumamosi, vijana wa Jacob ‘Ghost’ Mulee watacheza mechi nyingine mbili za kirafiki dhidi ya majirani Tanzania mnamo Machi 15 uwanjani Nyayo na Machi 18 ugani Kasarani.
Harambee Stars itaalika Mafirauni wa Misri mnamo Machi 25 kwa mechi yake ya tano ya Kundi G ya kufuzu kushiriki Kombe la Bara Afrika (AFCON) halafu ielekee Togo kwa mchuano wake wa mwisho utakaochezwa Machi 30.
“Mechi hizo zitatumiwa kujipiga msasa kabla ya zile za kufuzu kushiriki Kombe la Dunia 2022 zitakazoanza Juni 2021,” Shirikisho la Soka Kenya (FKF) lilisema Alhamisi.
KIKOSI
Makipa
Brian Bwire (Kariobangi Sharks), James Saruni (Ulinzi Stars), Joseph Okoth (KCB), Peter Odhiambo (Wazito), Sam Adisa (Bidco);
Mabeki
Johnstone Omurwa (Wazito), Michael Kibwage (Sofapaka), Samuel Olwande (Kariobangi Sharks), Nahashon Alambi (KCB), Bonface Onyango (Kariobangi Sharks), David Owino (KCB), Daniel Sakari (Kariobangi Sharks), Baraka Badi (KCB)
Viungo
Lawrence Juma (Sofapaka), Kenneth Muguna (Gor Mahia), Collins Shichenje (AFC Leopards), Micheal Mutinda (KCB), Musa Masika (Wazito), John Macharia (Gor Mahia), Reagan Otieno (KCB), James Mazembe (Kariobangi Sharks), Oliver Maloba (Nairobi City Stars), Bonface Muchiri (Tusker), Kevin Kimani (Wazito), Abdalla Hassan (Bandari)
Washambuliaji
Erick Kapaito (Kariobangi Sharks), Elvis Rupia (AFC Leopards), Henry Meja (Tusker), Benson Omalla (Gor Mahia)