Na GEOFFREY ANENE
KABRAS Sugar imerejea kileleni mwa Ligi Kuu ya raga nchini (Kenya Cup) baada ya kulipua wenyeji Kenya Harlequin 43-5 uwanjani RFUEA jijini Nairobi, Jumamosi.
Wanasukari wa Kabras kutoka Kaunti ya Kakamega walisalia wachezaji 14 uwanjani mapema baada ya Derrick Ashiundu kupata kadi nyekundu wakiongoza 7-0 kupitia mguso wa George Nyambua na mkwaju wa raia wa Fiji, Ntabeni Dukisa.
Walifungwa mguso bila mkwaju kutoka kwa Roxy Suchi baada tu ya adhabu hiyo, lakini wakajinyanyua na kuongeza miguso kupitia kwa Felix Ayange (miwili), Alfred Orege, Brian Tanga na Walter Okoth na mikwaju ya Dukisa.
Ni mara ya kwanza Kabras walifungwa mguso baada ya kupepeta Chuo Kikuu cha Masinde Muliro (MMUST) 56-0 na Leos ya Chuo Kikuu cha Strathmore 35-9 katika mechi mbili za kwanza.
Majirani wa Kabras, MMUST pia walikuwa na siku nzuri uwanjani hapo Jumamosi baada ya kushangaza miamba wa Mwamba 12-6 uwanjani KCB Ruaraka ambako pia wenyeji KCB walikung’uta Blak Blad ya Chuo Kikuu cha Kenyatta 32-19.