Na JOHN KIMWERE
JUMLA ya mechi nne zimepangwa kuchezwa wikendi hii kwenye mfululizo wa migarazano ya kufukuzia taji la Koth Biro makala ya 43 zitakaopigiwa uwanjani Umeme Ziwani, Nairobi.
Kwenye ratiba ya mechi za Kundi H, Leads United itateremka dimbani kuchuana na Huruma Corner FC huku mabingwa watetezi, Dallas Allstars ikionana uso kwa macho na Digo United. Kesho Jumapili, Wenyeji United imepangwa kucheza na Eastleigh Stars kwenye mechi za Kundi A.
Katika ratiba ya michuano ya Kundi B, Ngara United itakutanishwa na 1000 Sportive FC. ”Tumeandaa wachezaji wetu tayari kuanza kampeni zetu kwa ushindi dhidi ya wapinzani wetu,” kocha wa Dallas Stephen Mbogo alisema na kuongeza kuwa katika mpango mzima wamepania kupambana mwanzo mwisho kwenye jitihada za kutetea taji hilo walilobeba muhula uliyopita.
Anashikilia kuwa licha ya kutofahamu mchezo wa wapinzani wao hawana hofu yoyote huku akitoa wito kwa vijana wake kutolaza damu dimbani. Kocha wa Leads United, Wilston Issa alisema “Tunalenga kujituma kwa udi na uvumba kuhakikisha tunafuzu kushiriki fainali ya ngarambe ya msimu huu.”
Kwenye matokeo ya mechi zilizochezwa Alhamisi Kundi D, Biafra Kamaliza ilibeba ufanisi wa mabao 2-0 mbele ya Macmillan. Nayo Ngara Youth ya Kundi F ilitoka nguvu sawa bao 1-1 na Rongai United. Ngarambe ya mwaka huu imevutia jumla ya timu 46 ambapo mshindi atatuzwa kombe la Sh300,000.
Nambari mbili atapokea Sh100,000, nambari tatu na nne watapongezwa kwa Sh 50,000 na Sh20,000 mtawalia.