• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:15 PM
Manchester United wakabwa koo na Fulham katika EPL uwanjani Old Trafford

Manchester United wakabwa koo na Fulham katika EPL uwanjani Old Trafford

Na MASHIRIKA

MKUFUNZI Ole Gunnar Solskjaer amekiri kwamba sare ya 1-1 waliyolazimishiwa na Fulham ligini mnamo Jumanne usiku ugani Old Trafford inastahili “kuwazindua” wanasoka wake wanaojiandaa kwa fainali ya Europa League msimu huu.

Mabingwa hao mara 20 wa taji la EPL wamepangwa kuvaana na Villarreal ya Uhispania kwenye fainali ya Europa League itakayowakutanisha uwanjani Gdansk, Poland mnamo Mei 26, 2021.

Mfumaji Edinson Cavani aliwaweka Man-United kifua mbele katika dakika ya 15 kabla ya Fulham ambao tayari wameteremshwa ngazi kutoka EPL hadi Ligi ya Daraja la Kwanza (Championship) kusawazishiwa na Joe Bryan katika dakika ya 76.

Mchuano huo ulihudhuriwa na mashabiki 10,000. Mbali na Cavani, wanasoka wengine wa Man-United waliomtatiza pakubwa kipa Alphonso Areola wa Fulham ni kiungo Bruno Fernandes, Marcus Rashford na Scott McTominay aliyeondolewa uwanjani katika kipindi cha pili baada ya kupata jeraha la kifundo cha mguu.

“Tuna kibarua kigumu dhidi ya Villarreal. Hiyo ni mechi itakayotupa fursa ya kuwapa mashabiki wetu kitu cha kujivunia msimu huu. Matokeo dhidi ya Fulham yanastahili kutuzindua na kutufanya kujituma hata zaidi katika mechi ijayo kabla ya fainali ya Europa League,” akasema Solskjaer ambaye ni raia wa Norway.

Man-United ambao kwa sasa wanashikilia nafasi ya pili jedwalini kwa alama 71, watafunga kampeni za EPL msimu huu dhidi ya Wolves uwanjani Molineux mnamo Mei 23. Fulham kwa upande wao watakuwa wenyeji wa Newcastle United ugani Craven Cottage.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Chelsea walipiza kisasi dhidi ya Leicester City na kujiweka...

Shughuli ya kuhesabu kura Juja yaendelea baada ya vurugu...