Na GEOFFREY ANENE
KIUNGO wa zamani wa Sofapaka FC Ronald Okoth ndiye balozi mpya wa kituo cha kukuza talanta ya soka ya Emerging Stars ambayo makao yake ni katika Shule ya Upili ya St Mary’s jijini Nairobi.
Okoth,32, ametwikwa majukumu hayo Februari 9, 2021. Alichezea Gor Mahia, Western Stima, Mathare United, KCB na Sofapaka katika kipindi cha miaka 13 kabla ya kuangika daluga zake mwisho wa msimu uliopita wa 2019-2020.
Okoth amekuwa akijihusisha na soka tangu kustaafu kwake akifanya kazi ya kuchanganua mechi kwenye vyombo vya habari pamoja na kusaidia miradi mbalimbali ya mashinani inayojihusisha.
“Ana digrii ya Sayansi kutoka Chuo Kikuu cha Kenya Methodist na anapenda kujishughulisha na ukuzaji wa mchezaji aliyekamilika pamoja na kutambua talanta mapema na kukuza talanta changa na kumfanya mtu anayefaa kazi hii ya balozi wa Emerging Stars,” akademia hiyo ilisema.
Kwa upande wake, Okoth alifurahia kuungana na kundi la wataalamu “walio na ari ya kukuza talanta katika nyanja mbalimbali kama kocha, balozi na skauti”. “Nasubiri sana kuanza kutafuta talanta na kukuza mastaa wa siku za usoni,” alisema.
Mkurugenzi msimamizi wa akademia hiyo Christine Ouko alisifu Okoth kama mmoja wa wachezaji wazuri wa kizazi chake na kuamini kuwa ujuzi wake katika soka “utakuwa mchango mkubwa kwa makinda, mastaa wanaoinuka”. “Nasubiri kwa hamu kubwa kuanza safari hii muhimu naye,” alisema.