• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 6:40 PM
Olunga afunga mabao 5 kuisaidia Al Duhail kuzamisha Al Sailiya 5-0

Olunga afunga mabao 5 kuisaidia Al Duhail kuzamisha Al Sailiya 5-0

Na GEOFFREY ANENE

MSHAMBULIAJI matata wa Kenya, Michael ‘Engineer’ Olunga alirejea kwa kishindo katika kikosi cha Al Duhail baada ya kuachwa nje mechi mbili zilizopita, akitinga mabao yote katika ushindi wa 5-0 dhidi ya wageni wao Al Sailiya kwenye Ligi Kuu ya Qatar ya msimu 2021-2022, Jumapili.

Olunga, ambaye alikosa michuano dhidi ya Al Arabi mnamo Septemba 16 na Al Gharafa mnamo Septemba 22, sasa amerukia juu ya jedwali la wafungaji kwa mabao saba kwenye ligi hiyo ya klabu 12.

Nahodha huyo wa timu ya taifa ya Kenya, ambaye ameanza msimu wake wa kwanza mzima na Al Duhail baada ya kuwasili katikati ya msimu 2020-2021 mwezi Januari, alifungua msimu kwa kutetemesha nyavu za Al Khor mara mbili katika ushindi wa 4-2 Septemba 12.

Si kocha Louis Castro wala Al Duhail ilitoa sababu yake ya kukosekana kikosini dhidi ya Al Arabi na Al Gharafa ambazo bado walishinda 2-1 na 3-1 mtawalia. Hata hivyo, haikujalisha aliporejea kikosini.

Baada ya Al Duhail kumaliza dakika 45 za kwanza bila bao dhidi ya Al Sailiya, Olunga aliitwa kusaidia mabingwa hao wa zamani kutafuta mabao na hakusikitisha.

Dakika 10 baada ya kujaza nafasi ya Abdeirahman Moustafa mwanzo wa kipindi cha pili, alikamilisha pasi safi kutoka kwa nahodha Almoez Ali kupitia mguu wake wa kulia.

Olunga aliongeza bao la pili alipopata pasi ndefu kutoka kwa Ferjan Sassi baada ya kuwazidi kasi mabeki wawili na kuchenga kipa kupitia mpira wa kichwa kabla ya kutikisa nyavu dakika ya 62.

Kisha, Olunga alipata ‘hat-trick’ yake dakika ya 68 alipokamilisha pasi iliyosukwa na Mohammed Alaaeldin. Goli la nne lilipatikana dakika ya 79 baada ya Olunga kukamilisha shuti ya Almoez iliyotemwa na kipa. Mfungaji huyo bora wa Ligi Kuu ya Japan mwaka 2020 alihitimisha dakika ya 85 baada ya kupasiana mpira vyema na Almoez.

Ushindi huo unahakikisha Al Duhail inasalia juu ya jedwali kwa alama 12. Al Duhail ilipoteza taji kwa A Sadd msimu uliopita ambao Olunga alichangia mabao tisa ligini na 19 katika mashindano yote.

You can share this post!

Jifunze kuoka keki ya kakao na vanilla

Corona ilipunguza kasi ya mbinu za kisasa za upangaji...