• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 3:42 PM
Olunga apimwa corona kujiandaa kwa Kombe la Dunia la Klabu

Olunga apimwa corona kujiandaa kwa Kombe la Dunia la Klabu

Na GEOFFREY ANENE

KLABU ya Al Duhail anayochezea nyota Mkenya Michael Olunga imepimwa virusi vya corona Jumatano ikisubiri kuanza kampeni yake ya Kombe la Dunia la Klabu hapo Februari 4.

Mabingwa hao wa Qatar ni wenyeji wa kindumbwendumbwe hicho kitakacholeta pamoja pia wafalme Bayern Munich (Bara Ulaya), Ulsan Hyundai (Asia), Palmerais (Amerika ya Kusini), Al Ahly (Afrika) na Tigres UANL (Amerika ya Kaskazini, Kati na Caribbean) kutoka Februari 4-11 jijini Al Rayyan.

Mshambuliaji matata Olunga pamoja na kikosi chote cha kocha Sabri Lamouchi walipimwa virusi hivyo katika hoteli yao. Timu zote zitakuwa zikipimwa mara kwa mara kuhakikisha usalama wa vikosi dhidi ya maambukizi ya virusi vya corona ambavyo vimeshika watu 152,095 nchini Qatar na kuua 249. Matokeo ya vipimo hivyo kambini mwa Al Duhail hayajatangazwa.

Hata hivyo, wawakilishi hao wa Qatar waliendelea kujipiga msasa kwa mechi yao ya kufa-kupona ya ufunguzi dhidi ya miamba wa Misri Al Ahly itakayosakatwa Alhamisi saa mbili na nusu usiku. Mchuano huo utakuwa sawa na robo-fainali. Utapigiwa uwanjani Education City. Al Duhail haijawahi kushiriki Kombe la Dunia la Klabu kwa hivyo ni mara ya kwanza kabisa itakuwa katika kiwango hicho cha mashindano.

Al Ahly si timu geni katika kipute hiki. Vijana wa Pitso Mosimane walishiriki makala ya mwaka 2005, 2006, 2008, 2012 na 2013. Mshindi wa mechi kati ya Al Duhail na Al Ahly itakayosimamiwa na raia wa Guatemala Mario Escobar, atakumbana na kibarua kingine kigumu dhidi ya miamba wa Ujerumani Bayern katika nusu-fainali mnamo Februari 7.

Mchezaji bora na mfungaji bora wa Ligi Kuu ya Japan 2020 Olunga ni mmoja wa wachezaji Al Duhail itategemea kutafuta kung’ara nyumbani.

Mechi ya kufungua mashindano haya itakutanisha Tigres kutoka Mexico na Ulsan ya Korea Kusini saa kumi na moja usiku Alhamisi uwanjani Al Rayyan.

Mshindi hapa atamenyana na Palmerais katika nusu-fainali mnamo Februari 7. Fainali ni Februari 11.

You can share this post!

Waigizaji wa Ukombozi Film wanavyonoa vipaji vya watoto...

Festus Mwoki ashinda mbio za nyika za Pwani