• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 7:50 AM
Williams Inaki wa Bilbao aweka rekodi ya kuchezeshwa katika mechi nyingi zaidi mfululizo kwenye La Liga

Williams Inaki wa Bilbao aweka rekodi ya kuchezeshwa katika mechi nyingi zaidi mfululizo kwenye La Liga

Na MASHIRIKA

FOWADI Inaki Williams wa Athletic Bilbao aliweka rekodi mpya ya kuwa mwanasoka ambaye sasa amewajibishwa katika michuano mingi zaidi ya Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga) kwa mfululizo baada ya kuwa sehemu ya kikosi kilichowapepeta Alaves 1-0 mnamo Ijumaa usiku

Sogora huyo raia wa Uhispania mwenye umri wa miaka 27 alichezeshwa katika mchuano wake wa 203 mfululizo dhidi ya Alaves na hivyo akavunja rekodi iliyokuwa iliyowekwa na beki wa zamani wa Real Sociedad, Juan Larranaga kati ya 1986 na 1992.

Williams alianza safari ya kuweka rekodi yake mnamo Aprili 20, 2016 na kufikia sasa, amepachika wavuni mabao 39 na kuchangia 25 mengine.

Wakicheza dhidi ya Alaves, bao la Bilbao ambao kwa sasa wanashikilia nafasi ya sita jedwalini kwa alama 13 lilifumwa wavuni na Raul Garcia dakika chache kabla ya kipenga cha kuashiria mwisho wa kipindi cha kwanza uwanjani San Mames kupulizwa.

Idadi kubwa zaidi ya mechi ambazo zimewahi kusakatwa na mchezaji mmoja kwa mfululizo katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) ni 310 na rekodi hiyo inashikiliwa na kipa Brad Friedel.

Miongoni mwa wachezaji wa ndani ya uwanja (ambao si makipa), rekodi hiyo inashikiliwa na Frank Lampard aliyewahi kuwajibishwa na Chelsea ligini mara 164 mfululizo kati ya Oktoba 2001 na Disemba 2005.

  • Tags

You can share this post!

Stoke City wakomesha rekodi ya kutoshindwa kwa West Brom...

Beki wa zamani wa Spurs na Liverpool, Steven Caulker,...