NA BENSON MATHEKA
NAIBU Rais Rigathi Gachagua na Mkuu wa Mawaziri Musalia Mudavadi wanaonekana kushindana vikali kila mmoja akiimarisha uungwaji mkono katika ngome yake huku tofauti kati yao zikisemekana kuongezeka.
Viongozi hao wawili wamekuwa wakikutana na viongozi kutoka ngome zao za kisiasa wakiwemo wale wa upinzani na kuhubiri umoja wakilenga kujiimarisha kama vinara wa jamii na maeneo yao.
Mnamo Jumatano, Bw Mudavadi alikutaka na wabunge 35 kutoka eneo la Magharibi, siku tatu baada ya Bw Gachagua kuanzisha juhudi za kuunganisha eneo la Mlima Kenya nyuma yake.
Bw Gachagua anasisitiza kuwa lengo lake ni kuhakikisha eneo hili linaunga mkono serikali ya Rais William Ruto. Tayari, amepata uungwaji kutoka kwa viongozi wa upinzani eneo la Mlima Kenya ambao wamemtambua kama kiongozi wa eneo hilo anayeshikilia wadhifa wa juu serikalini.
Imeibuka kuwa Bw Gachagua na Bw Mudavadi wanajiandaa mapema kwa uchaguzi mkuu wa 2027 kila mmoja akipania kumhakikishia Rais Ruto kwamba, ana wafuasi wengi na uwezo wa kuunganisha ngome yake.
Mbunge wa Westlands, Bw Tim Wanyonyi akiwa mmoja wa waliohudhuria mkutano wa chamcha ulioitishwa na Bw Mudavadi alisema kwamba, hakuna kosa lolote viongozi wa Magharibi wakiungana nyuma ya kiongozi huyo wa chama cha Amani National Congress (ANC) kuweka mikakati ya kuhudumia wakazi.
“Kuna ubaya wowote Mudavadi akiunganisha eneo la Magharibi? Kila mwanasiasa huwa na azma na ikiwa anataka kuunganisha eneo lake inaanza namna hiyo kuwa siasa huanzia nyumbani na iwapo Musalia ataelekea njia hiyo, basi tutamuunga mkono,” Bw Wanyonyi alinukuliwa akisema.
Bw Mudavadi na Bw Gachagua wanaonekana kushindana ni nani kati yao anaweza kushawishi wabunge wengi wa upinzani kushirikiana na serikali ya Kenya Kwanza.
Rais Ruto amekuwa akihimiza viongozi wa Kenya Kwanza kuvuruga upinzani na kuhakikisha ajenda za kisheria za serikali zinapitishwa bungeni.
Bw Gachagua anasisitiza kuwa, lengo lake ni kuunganisha eneo la Mlima Kenya kuwa nyuma ya Rais Ruto akisisitiza kuwa msimu wa siasa umepita.
Akiwa kaunti ya Nyeri Jumapili iliyopita, Bw Gachagua alisema kufikia Desemba 31 2022, atakuwa ameunganisha viongozi wote nyuma ya Rais Ruto.
“Hapa mlimani tumeongea na viongozi na tumejipatia makataa ya Desemba 31 na waliokuwa wamepotoka na kuingia Azimio, tutawaleta nyuma ya William Ruto ndio mlima na Kenya isonge mbele,” alisema.
Duru zinasema kuwa ushindani kati ya viongozi hao wawili umemfanya Bw Mudavadi kukosa afisi tangu alipoapishwa mwezi Oktoba.
Awali, Mudavadi alipangiwa kuwa na ofisi katika Harambee House Annex ambako kuna afisi ya Naibu Rais, pendekezo ambalo Bw Gachagua alikataa.
Bw Mudavadi alitengewa afisi katika jumba la Shirika la Reli la Kenya ambazo zinaendelea kukarabatiwa.
Ingawa Bw Mudavadi alipohojiwa na Bunge la Taifa alisema hakungekuwa na mkanganyiko wa majukumu yake na yale Bw Gachagua alitengewa, wasaidizi wa Mkuu wa Mawaziri wanasema tofauti ya majukumu yao haijabainika vyema.
Wanataja jukumu la Mudavadi la kushirikisha ajenda ya kisheria kati ya wizara na idara zote na viongozi wa vyama na wa muungano tawala na jukumu la Gachagua la kusimamia utekelezaji wa maamuzi ya Baraza la Mawaziri katika wizara zote kama yanayozua ushindani kwa kufanana.
Subscribe our newsletter to stay updated