• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 3:42 PM
JAMVI: Njama ya Raila kubomoa One Kenya Alliance

JAMVI: Njama ya Raila kubomoa One Kenya Alliance

Na BENSON MATHEKA

KIONGOZI wa chama cha ODM, Raila Odinga, ameanza mikakati ya kuwapiga vita vya kisiasa vinara wenza katika National Super Alliamce (NASA), muungano aliotumia kugombea urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2017, ambao wameungana chini ya muungano wa One Kenya Alliance.

Mikakati yake inahusisha kubomoa muungano wa One Kenya Alliance ambao unashirikisha kiongozi wa chama cha Wiper Stephen Kalonzo Musyoka, Musalia Mudavadi wa Amani National Congress, Moses Wetangula wa Ford Kenya na Gideon Moi wa Kanu hata kabla haujatamba.

Katika juhudi zake za kuubomoa muungano huo, Bw Odinga ameanza kumshawishi Bw Moi kujiunga naye katika hatua za kuwatenga Bw Musyoka, Bw Musalia na Bw Wetangula ambao ni washirika wake katika NASA.

Watatu hao walimtenga Bw Odinga wakidai alisaliti mkataba wa NASA kuhusu ugawaji wa mapato na nyadhifa bungeni pamoja na kuunga mmoja wao kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka ujao.

Mapema wiki hii, Bw Odinga alikutana na Bw Moi na Bw Muhoho Kenyatta ambaye ni kaka mdogo wa Rais Uhuru Kenyatta katika kile ambacho wadadisi wa siasa wanasema ni mipango yake ya kuwatenga Musyoka, Mudavadi na Wetangula.

Bw Moi ana uhusiano wa karibu na Rais Kenyatta, kinara mwenza wa Bw Odinga katika handisheki. Inasemekana Muhoho ni mmoja wa washauri wa kaka yake mkubwa Rais Kenyatta.

Ingawa Muhoho hajawahi kuhusika moja kwa moja na siasa, wadadisi wanasema ni mmoja wa wanaotekeleza jukumu muhimu kupanga siasa za urithi baada ya kaka yake kustaafu 2022. Tangu handisheki amekuwa akimchangamkia Bw Odinga.

Duru za kisiasa zimekuwa zikidai kwamba Rais Kenyatta anapendelea muungano wa One Kenya Alliance jambo ambalo limezua minong’ono katika ODM kwamba anamsaliti Bw Odinga baada ya kumsaidia kumzima naibu wake William Ruto kupitia handisheki.

Dalili zinaonyesha kuwa Bw Odinga anavuruga ngome za Bw Musyoka, Bw Mudavadi na Bw Wetangula ili kuwanyima umaarufu waliofurahia baada ya chaguzi ndogo za hivi majuzi ambazo waliungana kubwaga ODM.

Katika ngome ya Bw Musyoka ya Ukambani, amemvuta Gavana wa Makueni Kivutha Kibwana upande wake. Kivutha ni hasimu wa kisiasa wa Bw Musyoka ambaye pia ametangaza azma ya kugombea urais kwenye uchaguzi mkuu wa 2022.

Mnamo Jumanne, Bw Odinga alituma ujumbe wa maafisa wa chama cha ODM kukutana na Profesa Kibwana kujadili uwezekano wa wawili hao kushirikiana kabla ya uchaguzi mkuu wa 2022.

Ujumbe huo ulioshirikisha maafisa wa ODM kutoka kaunti za Ukambani Makueni, Kitui na Machakos ulisema kwamba ulimrai Gavana Kibwana kushirikiana na Bw Odinga.

Katika ishara kwamba aliunga hatua ya Bw Odinga ya kumzima Bw Musyoka, Profesa Kibwana alimtaka waziri huyo mkuu wa zamani pia kuzungumza na mwenzake wa Machakos Alfred Mutua na Charity Ngilu wa Kitui.

Alifichua kwamba alikuwa amezungumzia suala la kubuni muungano wa kisiasa na Bw Odinga walipokutana mapema mwaka huu.

Bw Kibwana na Bw Mutua wanaohudumu kipindi chao cha mwisho cha ugavana ni wakosoaji wakubwa wa Bw Musyoka.

Katika eneo la Magharibi ambalo ni ngome ya kisiasa ya Bw Mudavadi na Bw Wetangula, Bw Odinga amemrai aliyekuwa katibu wa shirika la umoja wa mataifa kuhusu biashara Mukhisa Kituyi kumuunga mkono.

Mnamo Februari, Bw Odinga alikutana na Dkt Kituyi na Gavana Kibwana na tangu wakati huo, minong’ono ya kuungana nao ilianza kushika kasi.

Dkt Kituyi anatoka Bungoma anakotoka Bw Wetangula na inasemekana Bw Odinga anawarushia chambo wanasiasa wengine wa kaunti hiyo.

Katika eneo la Magharibi, Bw Odinga ameimarisha usuhuba wake na Gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya na inasemekana amekuwa akiwarushia chambo wanasiasa wengine wa eneo hilo walio na ushawishi mkubwa mashinani.

Wandani wa Bw Odinga wanasema kwamba ameanza njama ya kuhakikisha kuwa Rais Kenyatta amebadilisha nia ya kuunga One Kenya Alliance kwa kuvuta Bw Moi upande wake.

Baadhi ya wadadisi wa kisiasa wanasema kwamba hii inatokana na tetesi kwamba washirika wa karibu wa rais wanataka Bw Moi kumrithi.

“Akifaulu kubomoa One Kenya Alliance kwa kuukosesha uungwaji mkono na Rais Kenyatta basi Bw Odinga atakuwa ameondoa kisiki katika azima yake ya kuingia ikulu. Hii haimaanishi itakuwa mteremko kwake hata akiungwa na Rais Kenyatta mwenyewe kwa sababu vinara wa One Kenya Alliance wanaweza kuungana na Naibu Rais Ruto na kumtoa jasho kwenye kampeni,” asema mdadisi wa siasa Lawrence Koech.

Mdadisi huyu anasema kwamba hatua ya Bw Odinga kumrai Bw Moi, inaonyesha kuwa hayuko makini kuungana na Dkt Ruto ilivyodaiwa.

Uwezekano wa Bw Odinga na Dkt Ruto kuungana uliibuka naibu rais alipokutana na Gavana Oparanya kaunti ya Narok wiki jana ambapo inasemekana walijadili siasa za urithi za 2022.

“Bw Odinga anataka kucheza pande zote na nia yake kuu ni kuvuruga mipango ya vinara wenza katika NASA ili wasiungwe mkono na Rais Kenyatta au kuungana na Dkt Ruto,” aeleza Koech.

You can share this post!

DINI: Penda kusema ukweli siku zote, njia ya mwongo ni...

JAMVI: Magavana ‘wanaofunga kazi’ wang’ang’aniwa na...