NA SAMMY WAWERU
MGOMBEA wa urais kwa tiketi ya chama cha United Democratic Alliance (UDA) katika uchaguzi mkuu wa Agosti 9 Dkt William Ruto amewasili katika ukumbi wa Bomas, Nairobi ambapo mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), Wafula Chebukati anatarajiwa kutangaza rasmi matokeo.
Akiandamana na mkewe, Bi Rachael Ruto na wandani wake, Dkt Ruto amefika saa tisa alasiri.
Wawaniaji wengine waliowasili Bomas ni George Wajackoyah na Waihiga Mwaure.
Wanasiasa, viongozi na wageni kutoka ndani na nje ya nchi wamekita kambi Bomas of Kenya wakisubiri matokeo ya urais kutolewa.
IEBC ilitoa notisi Jumatatu, ikisema itatangaza rasmi aliyeibuka mshindi kinyang’anyiro cha urais mwendo wa saa tisa lakini shughuli hiyo imecheleweshwa kiasi.
Wagombea wanne: Raila Odinga (Azimio), William Ruto (Kenya Kwanza), George Wajackoyah (Roots Party) na David Mwaure wa Agano Party, walimenyana debeni.
Bw Raila wa ODM na Dkt Ruto (UDA) ambaye pia amehudumu kama naibu rais tangu 2013 ndio walikuwa wawaniaji wenye ushawishi mkuu.