• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 1:14 PM
Ruto kimya Mariga akihangaika

Ruto kimya Mariga akihangaika

Na BENSON MATHEKA

NAIBU Rais William Ruto jana alizidisha kimya chake huku hatima ya mwaniaji wa Chama cha Jubilee kwenye uchaguzi mdogo wa eneobunge la Kibra, McDonald Mariga, ikizidi kutiliwa shaka.

Tofauti na awali ambapo Dkt Ruto alijitokeza wazi na hata kuelekea Kibra kuahidi angerejea kuongoza kampeni za Bw Mariga, amekuwa kimya tangu wikendi kabla mwaniaji huyo kupigwa breki na Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Jumanne.

Bw Mariga alipokezwa cheti chake cha chama na Katibu Mkuu wa Jubilee, Bw Raphael Tuju tofauti na wagombeaji wa vyama vingine waliopokezwa vyeti na vinara wa vyama vyao.

Wakati alienda kuwasilisha stakabadhi zake kwa IEBC, aliandamana na wandani wa Dkt Ruto, akiwemo mbunge wa Langata, Nixon Korir, na aliyekuwa Seneta wa Kakamega, Dkt Boni Khalwale.

IEBC ilisema Bw Mariga hakuwa amesajiliwa kama mpiga kura nchini na hivyo basi, kisheria hawezi kuruhusiwa kuwania ubunge.

Vilevile, kuna tetesi zilizoibuka kuhusu umri halisi wa nyota huyo wa soka ikidaiwa huenda suala kuhusu uhalali wa kitambulisho chake pia likawa kikwazo kwa azimio lake la kujitosa kwenye ulingo wa siasa.

Jana, Bw Mariga alimshtaki Msimamizi wa Uchaguzi wa eneo hilo Bi Beatrice Muli mbele ya kamati ya kutatua mizozo ya IEBC akimlaumu kwa kukataa kumuidhinisha kugombea uchaguzi huo licha ya kuteuliwa na chama cha Jubilee.

Bi Muli alikuwa amesema hangempitisha Bw Mariga kuwania ubunge kwa kuwa jina lake halikupatikana katika sajili ya wapigakura iliyochapishwa 2017.

Hata hivyo, Bw Mariga anasisitiza kuwa amesajiliwa kisheria kama mpigakura na hatua ya Bi Muli ilikiuka haki zake za kikatiba.“Nilisajiliwa kama mpigakura katika kituo cha kupigia kura cha ukumbi wa kijamii wa Kariokor mnamo Agosti 26, 2019 na nikapatiwa kadi ya kuthibitisha nambari yangu ya mpigakura,” alisema Bw Mariga kwenye hati ya kiapo aliyoambatishwa na ombi lake.

Mwanasoka huyo mstaafu anasema kwamba, kabla ya kuteuliwa, Chama cha Jubilee kilithibitisha kwamba alikuwa ametimiza mahitaji yote ikiwa ni pamoja na kusajiliwa rasmi.

“Nimefahamishwa na wakili wangu na ninaamini ni kweli kwamba usajili wa wapigakura ni shughuli inayoendelea na kwamba majina huwekwa katika sajili kila wakati kwa mujibu wa sheria husika,” anasema.Bw Mariga anataka kamati kuamua kuwa hatua ya Bi Muli haikuwa na msingi wa kisheria na kwa hivyo ni batili.

Dkt Ruto alionekana hadharani mara ya mwisho Jumapili alipozuru Kaunti ya Kirinyaga. Kwenye mitandao yake ya kijamii, hajasema lolote kuhusu masaibu ya Bw Mariga isipokuwa mapema Jumanne alipokashifu vyombo vya habari kwa kudai kuna mpasuko chamani mwake kuhusu uwaniaji kiti Kibra.

Jana, wengi walitarajia angeandamana na Rais Uhuru Kenyatta aliyekuwa katika ngome yake ya kisiasa ya Eldoret kusimamia mahafali ya wanajeshi, lakini hakuwepo.

Bw Mariga anataka kamati ya IEBC kutambua na kuamua kwamba aliteuliwa kihalali na chama cha Jubilee na anastahili aruhusiwe kugombea kiti cha eneobunge cha Kibra kwenye uchaguzi mdogo wa Novemba 7.

You can share this post!

Morani anayesuka hela ndefu kwa kusonga nywele

BONGO LA BIASHARA: Vijana mafundi wa fanicha zinazopata...

adminleo