Na BENSON MATHEKA
GAVANA wa Kirinyaga Anne Waiguru amepata marafiki wapya wa kisiasa baada ya kutangaza nia yake ya kujiunga na chama cha United Democratic Alliance (UDA) cha Naibu Rais William Ruto.
Bi Waiguru ameonekana akitangamana na wafuasi wa Dkt Ruto ambao walikuwa mahasimu wake wakati wa kupigia debe mchakato wa kubadilisha katiba wa Mpango wa Maridhiano (BBI).
Kwenye kampeni hizo, gavana huyo alikuwa akimkosoa vikali Dkt Ruto na washirika wake akiwalaumu kwa kumdharau Rais Uhuru Kenyatta kwa kutounga BBI na handisheki yake na kiongozi wa ODM Raila Odinga.
Mnamo Alhamisi, alikutana na Seneta wa Nakuru Susan Kihika, mbunge wa Malindi Aisha Jumwa na mwakilishi wa wanawake wa kaunti ya Nyeri Rahab Mukami na akatangaza kuwa ameanza kupata marafiki wapya.
“Nikiwa na wanawake wenzangu, mahusiano mapya, ninaendelea kusikiliza,” Bi Waiguru aliandika kwenye anwani yake ya Twitter ambayo alichapisha picha akiwa na washirika hao watatu wa Dkt Ruto.