• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 8:55 PM
Wakereketwa wa BBI waomba kukubaliwa kucheza reggae

Wakereketwa wa BBI waomba kukubaliwa kucheza reggae

Na JUMA NAMLOLA

KIONGOZI wa ODM Raila Odinga anataka Mahakama ya Rufaa iruhusu kufanyika kwa kura ya maamuzi kuhusu BBI, wakati kesi ya kupinga mchakato huo inapoendelea kusikizwa.

Kwenye ilani ambayo Bw Odinga ameandaa kwa ajili ya kuwasilishwa katika Mahakama ya Rufaa kupinga uamuzi wa Mahakama Kuu uliozima mchakato wa BBI, anasema shughuli hiyo isipoendelea itatumbukiza Kenya kwenye mgogoro wa kikatiba.

Kulingana na nakala zilizoandaliwa na wakili Paul Mwangi kwa niaba ya Bw Odinga na sekretariati ya BBI, shughuli hiyo ina umuhimu mkubwa wa kikatiba na hivyo inabidi iendelee kama ilivyopangwa.

“Shughuli ya kubadilisha Katiba ina kazi nyingi kwani ina muda mahsusi unaofaa kuzingatiwa. Hivyo ni muhimu kuhakikisha kuwa nia ya walioanzisha mchakato huu inaheshimiwa,” anasema Bw Odinga kwenye ombi lake.

Anasema Wakenya watapata hasara kubwa iwapo Mahakama ya Rufaa haitabatilisha uamuzi wa majaji watano wa Mahakama Kuu, uliosimamisha marekebisho hayo ya Katiba kupitia BBI.

Pia anasisitiza kuwa mchakato huo haukuanzishwa na Rais Uhuru Kenyatta kama walivyoamua majaji wa Mahakama Kuu, mbali na Mbunge wa Suna Mashariki Junet Mohamed na aliyekuwa mbunge wa Dagoretti Dennis Waweru.

Bw Odinga anasema Mahakama Kuu ilijitwika mamlaka ya Wakenya milioni tatu waliotia saini kuidhinisha mchakato huo, jambo analoamini ni ukiukaji wa Katiba.

“Mahakama kimakusudi, ilipuuza ushahidi uliowasilishwa kuonyesha watu milioni tatu waliidhinisha marekebisho ya Katiba baada ya kuusoma na kuuelewa mswada wa BBI 2020,” inasema ilani hiyo ya rufaa.

Ilani hiyo ya rufaa yenye kurasa 438, inatoa sababu kadhaa zinazowakosoa majaji waliotoa hukumu ya kuzima rege ya BBI.Inasema walitoa uamuzi wao wakati ambapo tayari Wakenya milioni tatu, Mabunge ya kaunti zaidi ya 40 na Bunge la Taifa na Seneti yalikuwa yameshapitisha mswada huo.

Mnamo Mei 13, majaji Joel Ngugi, George Odunga, Jairus Ngaah, Chacha Mwita na Teresia Matheka walitupilia mbali mswada wa marekebisho ya Katiba kupitia BBI. wakisema unakiuka Katiba.

You can share this post!

Uhuru na Ruto wajiuzulu ikiwa hawawezi kushirikiana –...

Wilbaro yazoa ufuasi Nyanza na Magharibi