• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 1:14 PM
Wanasiasa wasukuma ngome zao kujisajili

Wanasiasa wasukuma ngome zao kujisajili

Na WANDISHI WETU

TUME Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) inaanza leo Jumatatu shughuli ya kusajili wapigakura kote nchini huku Naibu wa Rais William Ruto na kiongozi wa ODM Raila Odinga wakiweka mikakati ya kuhakikisha wanapata wapigakura wapya wengi katika ngome zao.

Dkt Ruto ameagiza wandani wake katika Bonde la Ufa, kuanzisha kampeni kabambe kuhakikisha kuwa vijana wanajitokeza na kusajiliwa kuwa wapigakura katika Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9, 2022.

Viongozi hao, wakiongozwa na maseneta Susan Kihika (Nakuru), Aaron Cheruyoit (Kericho); wabunge David Gikaria (Nakuru Mjini Mashariki), Liza Chelule (Nakuru), Samuel Tonui (Kuresoi Kusini), Samuel Gachobe (Subukia), Soipan Tuya (Narok); na magavana Hillary Barchok (Bomet), Paul Chepkwony (Kericho), wanaamini hatua hiyo itasaidia Dkt Ruto ambaye ametangaza kuwania urais kujipatia kura nyingi katika uchaguzi mkuu ujao.

Bi Kihika alifichua kuwa kampeni hiyo inaendelea katika kaunti zote za Bonde la Ufa, ikiwemo Narok na Kajiado.

Wandani wa Rais Uhuru Kenyatta na Bw Odinga, wakiongozwa na Gavana Lee Kinyanjui na mbunge wa Nakuru Mjini Magharibi Samuel Arama, pia wameanzisha kampeni ya kuhimiza vijana kuenda kujisajili kuwa wapigakura.

Wandani wa Dkt Ruto wanalenga kuhakikisha kwamba angalau watu 809,583 wanasajiliwa kuwa wapigakura katika eneo la Bonde la Ufa.

Shughuli ya kusajili wapigakura wapya kwa wingi inang’oa nanga leo Jumatatu na itaendelea hadi Novemba 2, 2021.

IEBC inalenga kusajili wapigakura wapya milioni 6 kabla ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2022.

Katika ngome ya Bw Odinga, Gavana wa Siaya Cornel Rasanga ameahidi kutunuku watu watakaosajiliwa kuwa wapigakura huku Gavana wa Kisii James Ongwae akitoa ahadi sawa na hiyo.

You can share this post!

TAHARIRI: Vijana wajisajili wasikike 2022

Ruto amlima Uhuru