• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Wanafunzi wa wazazi wasio na karo wasifukuzwe shuleni – Serikali

Wanafunzi wa wazazi wasio na karo wasifukuzwe shuleni – Serikali

MWANGI MUIRURI na DIANA MUTHEU

SERIKALI imetangaza kwamba itawachukulia hatua walimu ambao watafukuza watoto shuleni kwa kukosa karo au sare mpya wakati shule zitakapofunguliwa Jumatatu.

Akizungumza akiwa Kaunti ya Murang’a jana, Waziri wa Elimu George Magoha alisema serikali inataka wanafunzi wote kurudi shuleni kwa asilimia 100.Alisema serikali imetekeleza jukumu lake la kupeleka madawati shuleni ilivyoahidi na kutoa Sh18.5 bilioni kwa shule za msingi na za upili kufadhili masomo.

Kulingana na Prof Magoha, kila idara ya serikali inatekeleza mchango wake kuhakikisha kanuni za kuzuia corona zitazingatiwa na watoto wote wamerudi shuleni.Naibu waziri wa elimu (CAS) Zack Kinuthia alisisitiza kwamba sare mpya za shule na karo hazitapewa kipaumbele wanafunzi watakaporudi shuleni kuanzia Jumatatu ijayo.

“Tumeagizwa kuhakikisha hakuna mwanafunzi atakayefukuzwa shuleni kwa sababu ya karo au kutokuwa na sare mpya kwa sababu hatufungui shule kwa mashindano ya utanashati au kuonyesha nguvu za kifedha,” alisema Bw Kinuthia.

Alisema wizara imepokea jumbe ambazo shule zimetumia wazazi kuwataka walipe malimbikizi ya karo na pesa za sare shule zikifunguliwa na kusema walimu waliotuma jumbe hizo hawakuagizwa na wizara.

Baadhi ya jumbe ambazo Taifa Leo iliona zinawaagiza wanafunzi wa shule za mabweni kulipa malimbikizi ya karo, kuwa na maski 50, pesa za kununua sare mpya shuleni na lita tatu za sanitaiza.

Ingawa aliwahimiza wale ambao hawakuathiriwa mno na janga la corona kulipa malimbikizi ya karo, waziri alisema wale ambao wanapitia hali ngumu baada ya kupoteza mapato wanaweza kulipa baadaye kwa awamu mradi tu wajue wanadaiwa.

Wakati huo huo, Baraza la Kitaifa la Ushauri kwa Waislamu (KEMNAC) limeiomba Wizara ya Elimu kuondoa karo ya muhula wa kwanza.

Akizungumza na waandishi wa habari katika hoteli ya Panaroma, katika kaunti ya Mombasa, mwenyekiti wa baraza hilo, Sheikh Juma Ngao alisema kama karo hiyo haitaondolewa, basi wazazi wakubaliwe kulipa karo polepole, kwani wameathirika na kuwepo kwa virusi vya corona nchini.

‘Karo ya shule ya muhula wa kwanza twaomba iondolewe. Kama haitaondolewa basi wazazi wanafaa kupewa nafasi walipe polepole pasi na watoto wao kufukuzwa nyumbani,’ akasema Sheikh Ngao.

Mwanachama wa KEMNAC, Sheikh Mohammed Juma alisema wazazi wengi bado wanahangaika kuwatafutia wanao chakula. Kulingana na Wizara ya Elimu, shule zinafaa kufunguliwa mnamo Januari 4, 2021.

You can share this post!

Ruto kuhudhuria sherehe za ushindi Msambweni leo

Viongozi wataka Mvurya avalie joho la Sultan