• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 10:15 AM
NDIO! HAPA WIZI TU

NDIO! HAPA WIZI TU

NA WANDERI KAMAU

RAIS Uhuru Kenyatta amekiri kuwa uporaji pesa ndani ya serikali yake ni wa kiwango cha kutisha.Akizungumza jana asubuhi kwenye mahojiano na vituo vya redio vya lugha ya Kikuyu, Rais Kenyatta alisema wale wanaodai kuwa BBI itagharimu pesa nyingi ndio waporaji wakubwa na huwa wanaiba takriban Sh2 bilioni kila siku.

“Zile fedha ambazo watu hao huwa wanapora kila siku zinazidi Sh2 bilioni. Watu hao ni bure! Wanataka kutwambia ooh, BBI itatumia Sh2 bilioni, mara Sh1 bilioni! Je, wao huwa wanatumia fedha ngapi kwa mwaka?,” akasema.

Rais alisema hayo alipokuwa akimkashifu naibu wake, William Ruto na washirika wake kuhusu gharama ya kuandaa kura ya maamuzi.

Kauli hiyo inazua maswali kuhusu anachofanya Rais Kenyatta kukomesha wizi huo ikiwa anajua kuna wezi wanaofirisisha nchi ndani ya utawala wake, pamoja na uwezo wa taasisi kama vile Idara ya Kuchunguza Uhalifu (DCI) na Tume ya Maadili na Kupambana na Ufisadi (EACC) kukabiliana na uhalifu huo.

Kukiri huko kumetokea wakati serikali inapokabiliwa na uhaba mkubwa wa fedha, ambapo imeshindwa kutuma fedha kwa serikali za kaunti kutokana na kupungukiwa kifedha.

Wizi huo wa kutisha unaeleza sababu ya baadhi ya watumishi wa umma na wanasiasa kuwa na utajiri wa ajabu, ambao wengi hawawezi kufafanua walivyoupata, huku wananchi wa kawaida wakikosa huduma za kimsingi kama afya bora, ajira, barabara na elimu bora.Rais Kenyatta alitumia mahojiano ya jana kuwasihi wakazi wa jamii yake ya Wakikuyu kuunga mkono BBI, akisema watajuta iwapo haitapita.

Aliirai ngome yake ya Mlima Kenya isifuate wanasiasa wanaopinga ripoti hiyo, akitaja urekebishaji wa Katiba kupitia BBI kuwa njia ya pekee itakayohakikisha eneo hilo limefaidika kimaendeleo.

“Ni muhimu tutwae kilicho chetu sasa kupitia BBI badala ya kupewa ahadi kuhusu mambo ambayo tutatimiziwa katika siku zijazo. BBI ndiyo njia ya pekee itakayohakikisha maslahi yetu yamezingatiwa hata ikiwa mmoja kutoka jamii yetu hatakuwa uongozini,” akaeleza.

“Nitasimama na ukweli kuwa lengo letu ni kupeleka fedha mashinani kuwasaidia wananchi. Lengo kuu la ripoti hii ni kurejesha pesa mashinani kwa wananchi,” akasisitiza.

KUPOTOSHA WAKENYA

Akaendelea: “Wanaozunguka nchini wakiipinga BBI wanapaswa kukoma kuwapotosha Wakenya kwa kuwapa propaganda ambazo hazina msingi wowote. Mabilioni ya fedha ambazo wamepora kupitia miradi ghushi zinazidi zile ambazo zitatumika kwenye kura ya maamuzi.”

Hatua ya Rais Kenyatta kuzungumza kwa Kikuyu kwenye redio za FM ilionekana kama juhudi zake kujaribu kuzima upinzani mkubwa wa BBI katika ukanda huo.

Viongozi wengi na wakazi katika ngome hiyo yake ya kisiasa wanailaumu serikali kwa kulipa kipao mbele suala la BBI, licha ya kudorora kwa sekta muhimu za kiuchumi hasa kilimo, wakisema inaonekana amewasahau.

Hali hiyo pia imewafanya baadhi ya viongozi kuhama mrengo wa Kieleweke ambao umekuwa ukimtetea rais na kujiunga na ule wa Tangatanga, unaompigia debe Dkt Ruto kwenye azma yake kuwania urais mwaka ujao.

Wiki mbili zilizopita, Seneta Maalum Isaac Mwaura alihama Kieleweke na kujiunga na Tangatanga, akisema wenyeji wanataka kusikia serikali ikielezea kuhusu mikakati ambayo itachukua kuboresha hali ya uchumi nchini.

Suala hilo ndilo pia aliangazia pakubwa Kiranja wa Wengi kwenye Seneti, Irungu Kang’ata, kwenye barua maalum aliyomwandikia Rais kuhusu hali ilivyo kwenye ngome yake.

Hapo jana Rais Kenyatta alikosoa kampeni zinazoendeshwa na Dkt Ruto za “hasla”, akizitaja kama hatari kubwa inayoweza kuizamisha nchi kwenye vita vya matabaka.“Huu ni mwelekeo unaoweza kutuzamisha kwenye janga hatari ambalo huenda ikawa vigumu kujitoa kama nchi,” akaeleza.

You can share this post!

Mambo ya msingi kufahamu katika uandishi wa insha bora

Magara naye aongoza chama chake katika upande wake Ruto