• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Joho na Kingi waongoza mipango ya kuhama ODM

Joho na Kingi waongoza mipango ya kuhama ODM

Na MOHAMED AHMED

MIPANGO ya viongozi wa kanda ya Pwani kujisimamia kisiasa inazidi kupamba moto huku ripoti zikionyesha kuwa kumekuwa na majadiliano ya viongozi hao kujiondoa katika chama cha ODM.

Magavana Hassan Joho na mwenzake wa Kilifi, Amason Kingi mnamo Jumatatu walikuatana na wabunge tarkriban 25 katika kikao cha faragha kilichofanyika kwa zaidi ya saa tano.

Mkutano huo ulifanyika katika mkahawa mmoja eneo la Nyali, ambapo majadiliano yalihusisha umoja wa Pwani na iwapo umoja huo unapaswa ufanyike wakati viongozi hao wapo ndani ya ODM ama wakiwa na chama chao kutoka Pwani.

Akizungumza na “Taifa Leo” jana, Bw Kingi ambaye ndiye alikuwa ameongoza kuandaa mkutano huo, alisema majadiliano hayo yalilenga umoja wa Pwani ambao hautaegemea upande wa kinara wa ODM Raila Odinga ama Naibu Rais William Ruto.

“Ajenda yetu kuu ilikuwa umoja wetu. Tumekutana na wabunge ili kuweka mikakati na kwa sababu hiyo hatutakuwa na muungano ambo utaegemea upande wa Bw Odinga ama upande wa Bw Ruto. Hii itakuwa ajenda ya Pwani,” akasema Bw Kingi katika mahojiano baada ya mkutano huo.

Viongozi wengi waliohudhuria mkutano huo ni wa kutoka ODM. Wabunge ambao wanamuunga mkono Dkt Ruto hawakuwepo kwenye mkutano huo.

Bw Kingi alisema kanda ya Pwani imeamua kuchukua mkondo wake wa kisiasa kwa sababu kwa muda mrefu eneo hilo limekuwa likiachwa nyuma kwa sababu ya kuwacha wengine kuwasimamia.

Alisema ili kuipa nguvu ajenda hiyo ya umoja wa Pwani, magavana wote sita wa kanda hiyo watakutana Februari 9 katika kaunti ya Taita Taveta kujadiliana kuhusu mpango huo.

“Tumekuwa tukiwakilishwa na ODM kama eneo lakini sasa tunataka kujiwakilisha wenyewe na kujisimami. Kwa muda mfupi ujao utaona matunda ya mikutano hii ambayo tumepanga,” akaongeza Bw Kingi.

Bw Joho juzi pia alisema kuwa ni wakati wa viongozi wengine wa chama cha ODM akiwemo Bw Odinga kumuunga mkono yeye katika azma yake ya kuwania Urais mwaka wa 2022.

You can share this post!

Mashirika yamlaumu DPP kwa kuondoa kesi dhidi ya polisi

Wanafunzi wafeli majaribio ya KCPE kwa wingi