• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 6:55 AM
Mudavadi sasa akimbilia baraka za wazee kabla ya Muhkisa Kituyi

Mudavadi sasa akimbilia baraka za wazee kabla ya Muhkisa Kituyi

Na DERICK LUVEGA

KIONGOZI wa Chama cha Amani National Congress (ANC), Bw Musalia Mudavadi, amekimbilia kukutana na wazee wa jamii ya Waluhya siku chache baada ya aliyekuwa waziri Mukhisa Kituyi kutangaza rasmi atakutana na wazee na wadau wengine wa jamii kabla aamue rasmi kama atawania urais nchini.

Bw Mudavadi aliomba radhi kwamba hajawahi kufanya kikao na wazee baada ya kupewa hadhi ya kuwa msemaji wa jamii ya Waluhya mnamo 2016.

Kiongozi huyo wa ANC alitawazwa kuwa msemaji wa jamii hiyo katika hafla iliyoongozwa na Katibu Mkuu wa Muungano wa Wafanyakazi Nchini (COTU) Francis Atwoli katika uwanja wa michezo wa Bukhungu, mjini Kakamega.

Hata hivyo, baraza la wazee wa jamii hiyo walimshauri Bw Mudavadi kupuuzilia mbali ujio wa Dkt Kituyi na aendelee na mipango yake kuwania urais katika uchaguzi mkuu wa 2022.

Mwenyekiti wa baraza hilo Philip Masinde, aliyeongoza mkutano huo nyumbani kwa kiongozi huyo wa ANC, Malulu, kaunti ya Vihifa, alisema hata ikiwa hatapata bahati ya kuunda serikali, eneo la magharibi linafaa kuwa mshirika mkuu katika serikali ijayo.

“Sharti tuunde serikali ijayo. Lakini ikiwa kwa bahati mbaya hatutafanikiwa kufanya hivyo, sharti tuwe ndani ya serikali ijayo,” Mzee Masinde akasisitiza

.“Zamani tulikuwa na zaidi ya mawaziri watano. Leo, tunaambiwa sisi ni jamii nambari mbili kwa ukubwa nchini lakini hatuna waziri kutoka magharibi,” akaongeza mwenyekiti huyo ambaye ni mwanasiasa mkongwe kutoka kaunti ya Busia.

Alimtaka Bw Mudavadi kwenda kutafuta wandani wengine kutoka kwa wanasiasa wenye maono sawa na yake katika maeneo mengine ya nchi.

“Tuko nyuma yake kwa dhati, kwa maneno na vitendo. Sasa wajibu wako kwenda huko nje kusaka marafiki zaidi watakaokuwezesha kutimiza azma yako. Sisi tutakuwakilisha hapa vijijini,” Mzee Masinde akaeleza.

Kauli ya Masinde ilijiri baada ya wanachama wa baraza hilo kuapa kuunga mkono azma ya Mudavadi kuwania urais licha ya kwamba eneo la magharibi linaendelea kutoa wagombeaji wapya wa urais.Wazee hao walisema enzi ambazo “watu kutoka nje” walizuru eneo la Magharibi kiholela na kupata kura za wakazi zimepita.

Walisema wanataka uongozi ambao utafufua uchumi wa eneo hilo walilosema umeathirika pakubwa.Kwa upande wake, mwenyekiti wa baraza la Wazee wa Jamii ya Teso Ptala Naibei alisema kabila lake linazongwa na changamoto nyingi lakini hawataelekeza lawama kwa mtu yeyote.Alisema kabila hilo ambalo linaishi katika kaunti ya Busia limechanganyikiwa kwani halijapata mwelekeo wa kisiasa.

“Kwa hivyo, namwomba Bw Mudavadi kuzuru eneo letu ili auze sera zake,” akasema Mzee Naibei.Kauli yake iliungwa mkono na mwakilishi wa jamii ya Sabaot Bw Peter Chepkurui ambaye pia alimtaka Bw Mudavadi kuzuru eneo la Mlima Elgon.

Kwa upande wake, aliyekuwa Meya wa Webuye Patrick Kilaka alishangaa ni kwa nini kiongozi huyo wa ANC ameshindwa kufuata nyayo za babake, marehemu Moses Mudamba Mudavadi.

“Mzee Mudavadi aliacha jina ambalo hatujui lilitokomea wapi. Tuko wengi lakini hatuna uongozi. Mudavadi anafaa kutupa na kutuonyesha njia,” akasema, akiongeza kuwa bila kiongozi huyo wa ANC eneo zima la magharibi halina uongozi wa kisiasa.

You can share this post!

Familia 100 zakesha kwa baridini baada ya nyumba zao...

JAMVI: Nyachae alivyomtayarisha Matiang’i kuwa...