• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
KINYUA BIN KING’ORI: Raia wasipotoshwe na siasa za BBI, wazingatie manufaa

KINYUA BIN KING’ORI: Raia wasipotoshwe na siasa za BBI, wazingatie manufaa

 Na KINYUA BIN KING’ORI

N I wazi kwamba Mswada wa Marekebisho ya Katiba (BBI) unaoongozwa na Rais Uhuru Kenyatta na Kiongozi wa ODM Raila Odinga, umepiga hatua moja mbele baada ya kuidhinishwa na mabunge mengi ya kaunti.

Kufuatia ushindi huo wa BBI mahasimu wa Naibu wa Rais Dkt William Ruto akiwemo Raila Odinga, wameoenakana kuchukua hatua hiyo kama ushindi kwao kisiasa.

Hata viongozi ambao wamekuwa wakitetea BBI kama Musalia Mudavadi (ANC), Kalonzo Musyoka (Wiper), Gideon Moi (Kanu) na Moses Wetangula(Ford Kenya), wameonekana hadharani wakishangalia mafanikio ya BBI.

Wameishi kumsuta Dkt Ruto kama kiongozi aliyeshindwa kushwawishi mabunge ya kaunti yaliyo ngome yake kisiasa wakitaja mfano mzuri ikiwa ni Bomet na Kericho.

Sasa, vinara hao wanatarajiwa kuendesha kampeni kote nchini kuanzia mwezi huu, hata kabla ya Bunge la Kitaifa na lile la Seneti kutekeleza wajibu wao wa kukubali au kukataa mswada huo.

Hata hivyo, hatua hiyo haifai kufasiriwa kwamba Dkt Ruto hana umaarufu mashinani.

Madiwani wametumia mamlaka yao kuamua kuunga mkono mswada huo, na hilo kufaulu ni baada yao kuahidiwa ruzuku ya Sh2milioni za kununua magari.

Hivyo, viongozi hao kaunti hawakupiga kura kwa kuvutiwa na mapendekezo yaliyomo katika BBI bali walinaswa na fedha za kununua magari ya kifahari.

Hata baadhi ya mabunge hayo, yalipitisha mswada huo bila kuzingatia umuhimu wa kushirikisha wananchi mashinani kutoa maoni yao.

Baadhi ya madiwani hata hawakuchukua muda kusoma na kuelewa mapendekezo yaliyomo kwenye mswada wa BBI na jinsi yatakavyofanyiwa mabadiliko bali walishinikizwa kisiasa kupitisha au kuipinga BBI.

Kufaulu kwa BBI haimaanishi kumkweza kiongozi yoyote kisiasa 2022, hata kura ya maoni tunayotarajia Juni, mwaka huu haitakuwa kigezo cha kupima atakayeingia ikulu 2022. Hivyo, Dkt Ruto ni maarufu mashinani si mwanasiasa wa kupuuzwa kwa kisingizio cha BBI kupitishwa.

Hata hivyo, baada ya BBI kupitishwa katika mabunge ya kaunti na hata ikifaulu katika Bunge la Kitaifa na Seneti, hakuna anayepaswa kujigamba kuhusiana na ufanisi wake.

Wanasiasa wakiendelea kuingiza siasa katika BBI wananchi watabakia kupotoshwa, na wakati wao wa kuamua katika kura ya maamuzi watapiga kura kuikubali au kuikataa BBI kwa kuzingatia siasa na propaganda badala ya kuangalia uzuri wa mswada huo kwao.

Siasa za Dkt Ruto na Odinga zitachangia wakenya wengi kushindwa kushiriki mdahalo huo kwa umakini na utulivu.

You can share this post!

WANDERI KAMAU: Hukumu ya Sarkozy isaidie Waafrika kufunguka...

CHARLES WASONGA: Wakuzaji kahawa wapate hamasisho kuhusu...