• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
UDAKU: Georgina hajachoka kumkazia Ronaldo wazae mtoto wa tano

UDAKU: Georgina hajachoka kumkazia Ronaldo wazae mtoto wa tano

Na CHRIS ADUNGO

MWANAMITINDO Georgina Rodriguez, 27, amekiri bado matamanio yake ni kumzalia staa Cristiano Ronaldo wa Juventus mtoto nambari tano.

Kidosho huyo mzawa wa Mexico na raia wa Uhispania alijaliwa mtoto wa kike, Alana Martina, miaka mitatu iliyopita.

Pia analea watoto wengine watatu wa dume lake hilo – Cristianinho, 10, pamoja na pacha Eva Maria na Mateo Dos Santos watakaohitimu miaka minne mwezi Juni.

Akihojiwa wiki jana na jarida la InStyle nchini Uhispania, Georgina aliungama kuwa ni muda tu kabla familia yake na Ronaldo kupanuka zaidi.

“Tungependa kupata watoto zaidi lakini tumeacha hilo lifanyike wakati wake. Ninavyojua ni kwamba haitakawia sana. Kila siku na Ronaldo ni baraka tele kwani tunafurahia maisha. Sijawahi kuona zaidi yake,” alideka Georgina.

“Asilimia 95 ya maisha yangu huwa ni kushughulikia masuala ya familia. Nina watoto wengi tayari na kila mmoja anahitaji kiwango sawa cha mapenzi kutoka kwangu. Wanapendeza sana na ndicho chanzo cha furaha yangu,” akaongeza mrembo huyo.

Mnamo 2017, Georgina alikiri kwamba asingetaka kabisa kupata watoto wengine chini ya kipindi cha miaka 10.

“Kulea si lelemama. Kunataka mwanamke mwenye bidii na moyo wa kujitolea. Hawa wanne wakikua na kukomaa kuwa watu wazima, sioni tena haja ya kutafuta mwingine,” akasema wakati huo.

Lakini mwanamitindo huyo alionekana kubadilisha wimbo mwishoni mwa mwaka jana, alipofichua kwamba angali na kiu ya kuwa mjamzito.

Mateo na Maria walizaliwa na mwanamke raia wa Amerika baada ya Ronaldo kutoa mbegu zake za kiume zilizokutanishwa na yai la kichuna mmoja mzawa wa Uhispania, aliyelipwa Sh2.8 bilioni.

Mwanamke aliyejitolea kubeba mimba hiyo mwishoni mwa Septemba 2016 alipokezwa kima cha Sh1.5 bilioni.

Ronaldo aliwahi pia kutumia kima cha Sh1.2 bilioni kulipia yai la mwanamke mmoja mzawa wa Mexico mnamo 2010.

Baada ya yai hilo kukutanishwa na mbegu za kiume za Ronaldo, nyota huyo alimpa mwanamke mwingine mwenye asili ya Mexico kima cha Sh1.4 bilioni kubeba ujauzito huo, ambao ulileta mwanambee wa Ronaldo, Cristianinho.

Martina ndiye mtoto wa pekee wa Georgina na Ronaldo, ambaye amekuwa akisisitiza kwamba analenga kupata jumla ya watoto saba ili idadi hiyo iwiane na namba ya jezi yake.

“Mshishangae kuniona hivi karibuni nikianza kuhudhuria kliniki nikijiandaa kumzalia Ronaldo mtoto wa tano,” ndiyo maneno yaliyoandikwa na Georgina – kipusa mzawa wa Mexico – kwenye mtandao wake wa Instagram wiki jana.

Georgina alianza kumfungulia Ronaldo buyu lake la asali mnamo 2016.

baada ya sogora huyo raia wa Ureno kutemana na mwanamitindo Cassandre Davis wa Amerika.

Mwanzoni mwaka 2020, Georgina alisema yuko tayari kumzalia Ronaldo watoto watatu zaidi ila kwa masharti. Mwanzo alitaka sogora huyo akome kuwasiliana mara kwa mara na wapenzi wake wa zamani wanaomtaka upya, kisha amtwae rasmi na kumfanya wake wa halali kwa kula yamini ya ndoa.

Ronaldo amewahi pia kutoka kimapenzi na warembo Ellen Santana, Andressa Urach, Gema Atkinson, Rosie Oliveira na Irina Shayk ambaye kwa sasa ni mama wa mtoto mmoja, Lea De Seine, na mke wa mwigizaji mzawa wa Amerika, Bradley Cooper, 46.

You can share this post!

MBWEMBWE: Kwa mkwanja wa Sh35 milioni kuvumisha bidhaa za...

Ubutu wa msimamo wa Ruto kuhusu mswada wa BBI