• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 7:55 AM
Raila, Uhuru waamua kupimana nguvu Kisii

Raila, Uhuru waamua kupimana nguvu Kisii

WYCLIFFE NYABERI na RUTH MBULA

VIONGOZI wa vyama vya Jubilee na ODM, wameamua kuweka kando umoja wao uliotokana na handisheki ili wapimane nguvu katika uchaguzi mdogo eneobunge la Bonchari, Kaunti ya Kisii.

Vyama hivyo viwili vimekuwa vikiepuka kushindana katika chaguzi nyingi ndogo hatua iliyoonekana kuwa njia ya kudumisha umoja kwa manufaa ya muafaka kati ya Rais Uhuru Kenyatta na kinara wa ODM Raila Odinga.

Hata hivyo, Jubilee ndicho chama cha hivi punde kumteua mwaniaji wake, baada ya kumpokeza tikiti aliyekuwa mbunge wa eneo hilo, Bw Zebedeo Opore.

Kupitia kwa barua iliyoandikwa na katibu mkuu wa Jubilee, Bw Raphael Tuju kwa mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), chama hicho kiliomba mwanasiasa huyo mkongwe aidhinishwe.

Bw Tuju alipuuzilia mbali barua nyingine iliyosambazwa mitandaoni ikidai kuwa Jubilee imeamua isiwe na mgombeaji.

Alisema barua hiyo ilikuwa feki na kusisitiza Bw Opore atapeperusha bendera ya Jubilee katika uchaguzi huo mdogo.

Wakazi wa Bonchari watapiga kura kumchagua mbunge mpya kwenye uchaguzi mdogo wa Mei 18, kufuatia kifo cha Oroo Oyioka aliyeaga dunia mwezi Februari. Marehemu Oroo alifariki katika Hospitali ya Aga Khan mjini Kisumu baada ya kuugua kisukari kwa muda mrefu.

Mwanasiasa huyo mkongwe sasa atamenyana na Bi Teresa Bitutu ambaye ni mjane wa marehemu Oyioka, aliyepewa tiketi ya chama kinachohusishwa na Naibu Rais William Ruto, United Democratic Alliance (UDA) na Mhandisi Pavel Oimeke atakayewakilisha chama cha ODM.

Bw Oimeke, ambaye anakabiliwa na mashtaka ya ufisadi alipokuwa mkurugenzi mkuu wa bodi ya kudhibititi kawi (EPRA), alijiuzulu wadhfa huo hivi maajuzi ili kujitosa kwenye ulingo wa siasa.

Jumatatu, naibu mwenyekiti wa Jubilee, Bw David Murathe alidokeza kuhusu kuteuliwa kwa Bw Opore.

Bw Murathe alitupilia mbali madai kuwa hatua ya Jubilee na ODM kusimamisha wagombeaji katika uchaguzi mmoja ni ishara kuwa handisheki kati ya Rais Kenyatta na Bw Odinga, imeingia doa.

“Uamuzi wa Jubilee na ODM kuwateua wagombeaji watakaoshindana hakutasambaratisha handisheki kwa kuwa kiti hicho kilitwaliwa na chama tofauti uchaguzi wa 2017. Hivyo basi, kiti hicho ni wazi kwa yeyote,” akasema Bw Murathe.

Marehemu Oroo alishinda kiti cha Bonchari kupitia chama cha Peoples Democratic Party (PDP) kinachoongozwa na Bw Omingo Magara.

PDP iliamua kutoteua mwaniaji na badala yake kikatangaza ushirikiano na UDA ili kumuunga mkono mkewe marehemu Oyioka, Bi Bitutu.

Wawaniaji wengine walioonyesha nia ya kumrithi marehemu Oyioka ni Bw Victor Omanwa wa Party of Economic Democracy, kiongozi wa vijana wa KANU Bonchari Douglas Ogari, Onkendi Ondieki miongoni mwa wengine.

You can share this post!

57 kuosha jiji kwa kukiuka kanuni za Covid

Kenya Airways yatangaza hasara kubwa ya Sh36.6b