• Nairobi
  • Last Updated March 19th, 2024 11:34 AM
Wakazi waikejeli serikali kusitisha usambazaji wa maji

Wakazi waikejeli serikali kusitisha usambazaji wa maji

NA KALUME KAZUNGU

WAKAZI wa vijiji vya Witu na viungani mwake wameikejeli serikali ya Kaunti ya Lamu kwa kusitisha ghafla huduma ya usambazaji maji kupitia lori vijijini mwao.

Wakazi hao, wengi wao wakiwa ni kutoka vijiji vya Dide Waride na Bulto walitisha kushiriki maandamano kupinga hatua hiyo ya kaunti kuondoa gari la kusambaza maji eneo hilo bila ya kuwashauri.

Zaidi ya familia 400 kwa sasa zimekuwa zikihangaika kutokana na ukosefu wa maji tangu lori hilo lilipositisha huduma zake karibu miezi miwili iliyopita.

Lori hilo lilikuwa likisambaza maji kwa wananchi kila wiki ili kusaidia kukabiliana na ukame ambao umechangia kushuhudiwa kwa uhaba mkubwa wa maji kwenye vijiji mbalimbali vya Lamu.

Wananchi na mifugo wanalazimika kutembea kwa miguu hadi mjini Witu, ambako ni karibu kilomita 16 ili kununua maji ya matumizi ya nyumbani ambayo huuzwa kwa bei ghali.

Wakazi sasa wanawashurutisha maafisa wa serikali ya kaunti ya Lamu kurejesha huduma ya kusambaza maji kupitia lori mara moja la sivyo washiriki maandamano barabarani ili kilio chao kisikike nchini.

Hassan Ali alisema wamechoka kukaa bila maji, hivyo akaisisitizia kaunti na wahisani kuwaonea imani na kuwapumzisha mahangaiko wanayopitia kila kukicha wakitafuta maji.

Mifugo kwenye kijiji cha Dide Waride na viungani mwake pia wameripotiwa kufariki kutokana na kiangazi na ukosefu wa maji.

“Ni mwezi karibu wa pili huu tangu lori la kusambaza maji lilipoondolewa eneo hili. Hatukuarifiwa kwa nini gari hilo lilikomeshwa kusambaza maji kijijini kwetu. Tunalazimika kutumia pikipiki kubeba maji kutoka Witu hadi Dide Waride, ambapo huwa tunalipa kati ya Sh 200 na Sh 400 ili kufikishiwa maji hapa. Kaunti itusaidie kutatua shida hii,” akasema Bw Ali.

Bi Fatma Said alisema mara nyingi wamelazimika kulala bila kula kutokana na uhaba wa maji unaoendelea kukumba eneo lao.

Bi Said alieleza kusikitishwa kwake na hatua ya kaunti ya kusitisha huduma ya kusambaza maji vijijini mwao.

“Tunalala kwa njaa kwa kukosa maji. Dide Waride ni mojawapo ya maeneo ambayo yanashuhudia ukame mkali kila mwaka. Ninashangaa kwa nini kaunti ikaamua kusitisha huduma hiyo ya kutusambazia maji kupitia lori hapa. Warekebishe hali hii. Tunaumia.” akasema Bi Said.

Kwa upande wake aidha, Waziri wa Masuala ya Huduma za Umma na Majanga ya Dharura wa Kaunti ya Lamu, Abdu Godana alipinga madai kuwa kaunti ilikuwa imesitisha huduma za kusambazia maji wakazi wa Dide Waride kupitia lori.

Badala yake, Bw Godana alisema mikakati inaendelea katika ofisi yake na kwamba kabla ya mwisho wa juma hili tatizo la maji kijijini Dide Waride litakuwa limeshughulikiwa.

Bw Godana alisema huduma za lori hilo la kubeba maji zilisitishwa kwa muda kijijini humo ili kupisha nafasi kwa wakazi wa kijiji cha Bar’goni, ambacho pia kinakabiliwa na uhaba wa maji wapate huduma hiyo.

Alisema idara yake ina mpango wa kuongeza malori yatakayokuwa yakisambazia wananchi maji vijijini hivi karibuni.

“Hatujaacha kusambazia wananchi maji. Gari ni moja na linasambaza maji vijijini kwa zamu. Juma lililopita na hata sasa lori limekuwa likisambaza maji Bar’goni, Basuba, Kiangwe na Kiunga. Tutarejelea usambazaji wa maji Dide Waride,Wit una viungani mwake kufikia kesho. Pia tuna mpango wa kuongeza malori hivi karibuni ili maji yasambazwe kila mahali bila kukoma,” akasema Bw Godana.

Juma lililopita, wakazi zaidi ya 3000 wa vijiji vya Siyu, Shanga-Rubu, Shanga-Ishakani na Pate, kaunti ndogo ya Lamu Mashariki walijitokeza kulalamikia uhaba wa maji ambao unakumba eneo hilo tangu msimu wa kiangazi ulipoanza Lamu na nchini kwa jumla.

You can share this post!

Mama Sarah Obama alikuwa mwanamke wa kipekee – Raila...

Taharuki watu watatu wakiuawa Kenol