• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:55 AM
Mhubiri Nyeri achoma karatasi za kutangaza huduma za waganga

Mhubiri Nyeri achoma karatasi za kutangaza huduma za waganga

Na SAMMY WAWERU

MHUBIRI mmoja eneo la Nyeri amewashangaza wenyeji kwa kuchoma karatasi zenye notisi za huduma za waganga zilizobandikwa katika maeneo ya umma, mabango na kwenye miti.

Mtumishi huyo wa Mungu na ambaye Taifa Leo imebaini anafahamaika kama Peter Gitahi, ameapa kuteketeza notisi zote Nyeri zinazotangaza huduma za uganga.

Pasta Gitahi ameendelea na hatua hiyo licha ya tetesi kuwa “ameonywa na baraza la waganga Nairobi”.

Juma hili, amekita kambi eneo la Chaka, picha zake akichoma notisi hizo zinazosambaa mitandaoni zikionekana kunaswa usiku.

“Anasaidia halmashauri ya jiji kusafisha mazingira. Matangazo yasiyolipiwa ada hayaruhusiwi,” #Fanuel Njiru akachangia kwenye Twitter, kufuatia chapisho analoonekana akichoma karatasi.

“Aache biashara za wenyewe zinawiri. Baadhi ya wahubiri pia wamegeuza nyumba ya Mungu kuwa biashara,” Monicah Peter akaandika, akizua ucheshi.

Duru zinaarifu Bw Gitahi ameapa kuendeleza oparesheni hiyo katika maeneo mengine ya nchi kama vile Mombasa.

“Sasa hapo pa Mombasa ajue hao si wachawi wa kawaida. Atakuwa anaona karatasi akienda kuitoa inageuka kuwa nyoka,” #Soni Sonee akazua ucheshi Facebook.

“Akija hapa Mombasa asahau Nyeri, kwa sababu hawa wa Mombasa ni moto wa kuotea mbali,” Jane Gicharu akatahadharisha.

  • Tags

You can share this post!

Gor na Leopards mashakani

Mwanabodaboda apigwa faini ya Sh11,000