• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 2:25 PM
TAHARIRI: Kudungwa chanjo hakutozuia corona

TAHARIRI: Kudungwa chanjo hakutozuia corona

KITENGO CHA UHARIRI

WAKATI huu ambapo baadhi ya kaunti zimefungwa kama njia ya kudhibiti maambukizi ya maradhi ya corona, Wakenya wengi wanaendelea kuathiriwa na uamuzi huo.

Ingawa kaunti zilizofungwa kwa sababu ya viwango vya juu vya ugonjwa huo ni; Nairobi, Kiambu, Machakos, Kajiado na Nakuru, karibu kaunti nyingine 42 zimeathiriwa.

Nairobi ndiyo inayounganisha reli ya kisasa (SGR) kutoka Mombasa. Safari za magari kati ya miji hiyo miwili zilisimamishwa.

Kufungwa huko kumesababisha kuathirika kwa sekta ya utalii. Zaidi ya wafanyakazi 4,000 katika hoteli za kitalii watapoteza kazi kufuatia uamuzi wa hoteli nyingi za Pwani kupanga kusitisha shughuli kwa miezi mitatu. Msambao wa homa hiyo umechangia hoteli kadha kukosa biashara wakati wa msimu wa Pasaka na hali inatarajiwa kuendelea kuwa mbaya.

Mkurugenzi Mkuu wa Muungano wa Waendeshaji Biashara za Hoteli (KAHC), tawi la Pwani Sam Ikwaye alisema sekta hiyo itaporomoka ikiwa Rais Kenyatta hatafungua nchi wiki chache zijazo.

Kulingana na afisa huyo, mwaka 2020, wafanyakazi walikamilisha likizo zao za kulipwa na kwamba wakati huu wamelazimika kuwapa likizo zisizolipiwa. Baadhi ya hoteli zenye vitanda 300 zimepata wageni 10 pekee, idadi ambayo haiwezi kuleta faida yoyote. Zilizoathiriwa zaidi ziko maeneo ya Mombasa, Diani, Watamu na Malindi.

Changamoto hii na nyingine zinapoendelea, imebainika kuwa baadhi ya watu waliopata chanjo wameamua kutozingatia kanuni za kuzuia ugonjwa huo.

Kuna watu wanaowalipa polisi kitu kidogo na kufumbiwa macho wanapoingia au kutoka maeneo yaliyofungwa. Unapofika kwenye vituo vingi vya safari za mbali jijini Nairobi, utawasikia watu wakinadi safari za kwenda Mombasa au Kisumu, huku maafisa wa polisi wakipita. Ujasiri wa aina hii unaonyesha kuna jambo wanalofahamu watu hao.

Vitendo hivi ni hatari kwa afya ya wahusika na watu wengine, hata wanaojichunga.

Majuzi, Gavana Kiraitu Murungi (Meru) na aliyekuwa gavana wa Nairobi, Dkt Evans Kidero, waliambukizwa corona hata baada ya kupata chanjo.

Wataalamu wanasema kwamba jambo hili halifai kuwashangaza watu. Kwamba huchukua muda wa wiki kadhaa kabla ya chanjo anayodungwa mtu kuanza kuupa mwili kinga inayohitajika. Kwa hivyo inawezekana mtu akachanjwa leo Jumapili na akapata corona Jumapili ijayo.

Isitoshe, wataalamu hao wanasema lengo la kupewa chanjo si kuzuia mtu kupata corona, bali kupunguza makali ya ugonjwa huo iwapo ataupata. Kwa mfano kama mtu angepata corona ya kulazimu alazwe ICU, akiupata baada ya chanjo atalazwa chumba cha wagonjwa wasiohitaji kuwekewa mitungi ya gesi.

You can share this post!

Sakaja amshukuru Rais Kenyatta kwa kutoa Sh1 milioni kumfaa...

Wahudumu 4,000 kupoteza kazi hoteli Pwani