• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 11:13 AM
Kiptanui na Tanui waibuka washindi wa Xiamen Siena Marathon

Kiptanui na Tanui waibuka washindi wa Xiamen Siena Marathon

Na GEOFFREY ANENE

ERICK Kiptanui alitawazwa mfalme mpya wa mbio za kilomita 42 za Xiamen Siena Marathon zilizofanyika nchini Italia, Jumamosi.

Taji la wanawake pia lilinyakuliwa na Angela Tanui (2:20:08) aliyefuatwa na Mkenya mwenzake Purity Changwony (2:22:46) na Muethiopa Gedamu Gebiyaneshayele (2:23:23) mtawalia.

Kiptanui, ambaye atafikisha umri wa miaka 30 hapo Aprili 19, alizoa ushindi baada ya kukamilisha umbali huo kwa saa 2:05:48 Jumamosi. Rekodi ya Xiamen Marathon ya saa 2:06:19 imedumu tangu Mkenya mwenzake Moses Mosop aweke mwaka 2015 nchini Uchina.

Kiptanui ni Mkenya wa kwanza kunyakua taji la Xiamen tangu Mkenya mwenzake Vincent Kipruto mwaka 2016.

Alijiweka pazuri kuzawadiwa Sh3.2 milioni za kutwaa taji hilo. Hatapata tuzo ya kuweka rekodi mpya ya Xiamen Marathon ya Sh1.9 milioni kwa sababu moja ya sheria za mbio hizo waandalizi wanasema ni kuwa mtu mmoja haruhusiwi kutuzwa mara mbili. Unaruhusiwa kuchukua tuzo ya juu. Ikiwa angevunja rekodi ya dunia ya saa 2:01:39 inayoshikiliwa na Mkenya Eliud Kipchoge angepokea bonasi pekee ya kufanya hivyo ambayo waandalizi walitangaza Januari kuwa Sh107.3 milioni.

Kiptanui alifuatwa na Muethiopa Abdi Nigassa (2:05:57), Mmoroko Othmane El Goumri (2:06:18), Yohane Ghebregeris kutoka Eritrea (2:06:28), Muethiopa Kebede Wami (2:06:32) na Mkenya Solomon Kirwa Yego (2:06:41) mtawalia.

Wakenya Lucas Rotich (2:07:23), Bethwell Rutto (2:07:41), Edwin Kimaru (2:07:51) na Bethwel Yegon (2:08:18) walinyakua nafasi ya 11 hadi 14 katika usanjari huo nao Michael Njenga (2:08:28) na Stanley Kiprotich Bett (2:08:57) wakaridhika na nambari 16 na 20, mtawalia.

Makala hayo ya 18 yalivutia wakimbiaji 12,000. Kiptanui na Tanui watapokea tuzo zao wakipatikana hawakutumia dawa za kusisimua misuli kupata mafanikio hayo.

You can share this post!

ANC yadai ODM inamtisha Uhuru kwa kutisha kuungana na Dkt...

Wanafunzi wa nchi za nje wapenda vyuo vikuu vya nchini Kenya