• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 10:50 AM
KAULI YA MATUNDURA: Mashekhe wanachangia kudorora kwa matokeo ya Kiswahili Pwani ya Kenya?

KAULI YA MATUNDURA: Mashekhe wanachangia kudorora kwa matokeo ya Kiswahili Pwani ya Kenya?

Na BITUGI MATUNDURA

KATIKA makala yangu yaliyochapishwa kwenye Taifa Leo Juni 16, 2021) niliahidi kuendeleza majadiliano ya wataalamu wa Kiswahili kuhusu chanzo cha matokeo duni ya Kiswahili katika mitihani ya taifa ya shule za msingi (KCPE) na upili (KCSE).

Mdahalo huo ulichukua mkondo ‘mpya’ baada ya msomi wa Kiswahili, Dkt Wambua Kyeu, anayefundisha Marekani kuibuka na nadharia tete kwamba hali hiyo huenda inachangiwa na mashekhe wanaohubiri misikitini kwa ‘kutumia lahaja’. Mdahalo huo ulifanyika katika ukumbi wa WhatsApp wa Chama cha Ukuzaji Kiswahili Duniani (CHAUKIDU).

Ikumbukwe kwamba lugha ya Kiswahili ina takriban lahaja 15. Lahaja hizi ni pamoja na Kiunguja (Zanzibar), Kimakunduchi (au Kihadimu) na Kitumbatu (kinachozungumzwa maeneo ya mashambani, Zanzibar), Kipemba (kisiwa cha Pemba); Kimtang’ata (Tanga); Kimrima (pwani ya Tanzania) na Kimgao (Kilwa).

Lahaja nyingine ni : Kimvita, Kingare na Kijomvu (kisiwani Mombasa na viunga vyake); Kiamu, Kisiu, Kipate, Kibarawa (Kimiini/Chimiini), na Kitikuu (pwani ya kaskazini ya Kenya hadi Somalia kusini), Kivumba na Chichifundi (Wasini na Vanga), Kingwana (DRC na Kongo) na Kingozi (Kiswahili asili).

Kiunguja ndiyo lahaja iliyoteuliwa na wamishionari mnamo miaka ya 1930 kuwa msingi wa usanifishaji wa Kiswahili. Katika mchakato wa uteuzi wa lahaja ya usanifishaji wa Kiswahili, kulikuwa na suala la kukidhi maslahi pamoja na siasa.

Mtaalamu Abdallah Khalid ameliangazia suala hili kwa uketo katika kitabu chake – The Liberation of Kiswahili from European Appropriation (East African Literature Bureau, 1977). Kiunguja ‘kilipendelewa’ kuliko Kimvita na lahaja nyingine kwenye kinyang’anyiro cha uteuzi wa lahaja ya usanifishaji kwa madai kwamba kilikuwa kinatumiwa sana katika shughuli za biashara na vilevile kuwa na maandishi mengi (written corpus). Aidha, mtaalamu Ireri Mbaabu ameandika kwa uketo jinsi Kiswahili kilivyosanifishwa katika kitabu chake – Historia ya Usanifishaji wa Kiswahili (TATAKI, 2007).

Fasiri ya kimsingi ya dhana ‘lahaja’ kwa mujibu wa wanaisimujamii ni: tofauti katika matamshi, maumbo na matumizi ya maneno katika maeneo mbalimbali yenye asili moja. Kutokana na ufafanuzi huu, wanaisimujamii hujipata taabani katika kuweka mpaka baina ya lugha na lahaja. Mumo kwa mumo katika lugha mna lahaja.

Ubainifu baina ya dhana hizi mbili unaweza kuonekana bayana tunapoangalia ‘lugha’ kwa mkabala wa siasa kimaeneo (Geopolitics of language). Kwa mfano, nchini Kenya, ingawa tuna jamii ya watu wanaoitwa Wameru, hakuna hata mmoja ‘anayeweza kuzungumza Kimeru’. Wanachozungumza watu wa jamii hii ni lahaja za Gichuka, Kimwimbi, Kitigania, Kiigembe, Kitharaka n.k. Kwa hiyo dhana ‘Kimeru’ imefumbata zaidi mwonoulimwengu wa eneo la kijiografia na kisiasa kuliko mwonoulimwengu wa lugha.

Hatua ya usanifishaji wa lugha yoyote ile haiwanyimi wala kuwazuia wasemaji wa lahaja fulani kuizungumza lahaja yao. Kinachosababishwa na shughuli ya usanifishaji ni kuweka tu mipaka ya kuonesha wazungumzaji wa lugha/lahaja ni lini, wapi na vipi wanapaswa kuzungumza lugha sanifu.

Kwa hiyo, nadharia tete ya Mwalimu David Wambua Kyeu kuwa hotuba za Sheikh Izudin Alwy Ahmed misikitini anayesema ‘moya’ badala ya ‘moja’, ‘kitwa’ badala ya ‘kichwa’, ‘ndia’ kwa maana ya njia ina suluhu katika Kiswahili sanifu.

Makala yataendelea…

You can share this post!

KINA CHA FIKRA: Kuteka watoto nyara ni unyama na hatari kwa...

GWIJI WA WIKI: Robert ‘Ramtez’ Elijah