• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:55 AM
Kaunti pwani zapigwa darubini kuhusu miradi hewa

Kaunti pwani zapigwa darubini kuhusu miradi hewa

Na WAANDISHI WETU

BAJETI ya Serikali ya Kaunti ya Tana River, imekosolewa baada ya kubainika kuwa Sh100 milioni zilitengwa kwa ujenzi wa makao makuu ya kaunti katika eneo tofauti na lile ambako ujenzi ulikuwa unaendelea awali.

Kulingana na bajeti hiyo, pesa hizo zitatumiwa kujenga makao makuu katika miji ya Garsen na Madogo. Hii ni licha ya kuwa, kuna ujenzi unaogharimu Sh200 milioni katika kijiji cha Dayate, eneobunge la Galole ambao umefadhiliwa na kaunti hiyo kwa ushirikiano na serikali kuu.

“Hakuna chochote kama makao makuu Garsen na Madogo, na hakuna ushahidi wowote wa ujenzi unaoendelea maeneo hayo ambao unahitaji kukamilishwa,” akasema Katibu Mkuu wa shirika la kijamii la Tana River Civil Association, Bw James Onchaga.

Kando na hayo, miradi mingine haijafafanuliwa itajengwa wapi na hivyo kuibua changamoto endapo kuna wananchi au mashirika huru ambayo yatataka kufuatilia utekelezaji.

Juhudi zetu kutafuta ufafanuzi hazikufua dafu kwani Waziri wa Fedha katika kaunti hiyo, Bw Mathew Babwoya hakushika simu wala kujibu ujumbe aliotumiwa.

Katika Kaunti ya Lamu, Sh33 milioni zilitengewa ujenzi wa makazi ya Gavana huku Sh38 milioni zingine zikitengwa kukamilisha ujenzi wa jengo la makao mkuu ya kaunti ya Lamu lililoko mjini Mokowe.

Katika Kaunti ya Mombasa, idara ya afya imetengewa asilimia 25 ya bajeti ya Sh14.3 bilioni, ambayo ni sawa na Sh3.6 bilioni. Imefuatwa na idara ya maji na usafi (Sh1.23 bilioni), ujenzi na uchukuzi (Sh1.19 bilioni) na elimu na teknolojia ya habari (Sh1 bilioni).

Ripoti za Stephen Oduor, Kalume Kazungu, Siago Cece, Wachira Mwangi na Alex Kalama

You can share this post!

Ni wizi wizi tu!

Italia kukutana na Uhispania kwenye nusu-fainali za Euro...