• Nairobi
  • Last Updated May 5th, 2024 7:50 AM
Jamii ndogo zataka Rais abuni wizara iwasaidie

Jamii ndogo zataka Rais abuni wizara iwasaidie

Na CECIL ODONGO

VUGUVUGU la Wasomi kutoka jamii ndogo zilizotengwa, limemrai Rais Uhuru Kenyatta kubuni wizara ambayo itayashughulikia haki zao likidai kubaguliwa kuhusu masuala mbalimbali nchini.

Wanachama wa vuguvugu hilo wanatoka katika jamii ndogo 79 kwenye kaunti 29 huku lengo lao kuu ni kuhakikisha matakwa yao yanazingatiwa na serikali kuu pamoja na zile za kaunti.

Viongozi wa kundi hili wakiongozwa na mlezi wake Amos Ole Mpaka, mwenyekiti Charles Nandaini na mwakilishi wa jamii ya Kiarabu katika Kaunti ya Wajir Khadija Mohamed, walisema kuwa wakati umewadia kwa jamii hiyo kupigania haki ili kunufaika kimaendeleo.

Bw Ole Mpaka alisema kutokana na utawala na ubabe wa jamii kubwa kubwa haswa, maslahi ya makabila madogo yamekosa huduma bora za kiafya, miundombinu, maji na pia mara nyingi wao hubaguliwa wakati wa utoaji wa ajira katika taasisi mbalimbali za serikali.

“Tunamwomba Rais abuni wizara au shirika ambalo litatusimamia kukomesha ubaguzi wa tangu jadi dhidi yetu. Hata baada ya ujio wa utawala wa ugatuzi, maazimio ya wawakilishi wetu huwa hayatiliwi manani kutokana na idadi yetu ndogo,” akasema Ole Mpaka katika mkahawa moja wakati wa kuzindua vuguvugu hilo.

Aidha walilaumu viongozi kutoka makabila makubwa kuwahadaa kupitia nafasi za uteuzi kisha kugeuka baadaye na kupuuza maslahi yao.

Hasa walitaja kuwa kutokana na idadi yao ndogo, huwa hawahusishwi hasa katika masuala ya upangaji wa miradi ya maendeleo.

“Ni kweli kwamba hatuwezi kushinda cheo chochote lakini tunapoafikiana na jamii kubwa kuhusu masuala ya uongozi, maelewano hayo yaheshimiwe na yasitumiwe kutudhalilisha,” akaongeza.

Diwani wa wadi ya Terik, Kaunti ya Nandi Osborne Komen alisimulia jinsi ambavyo mswada wake wa kupendekeza ujenzi wa Chuo cha Mafunzo ya Ufundi ulivyoangushwa na madiwani kutoka jamii kubwa, huku akitoa wito nafasi nyingi za uteuzi zitolewe kwa jamii ndogondogo.

You can share this post!

TANZIA: Hillary Ng’weno afariki, aacha historia ya...

Saburi kusalia ODM wenzake wakihepa