• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
KINYUA BIN KING’ORI: Wanasiasa wajiepushe na mjadala wa kuahirisha uchaguzi

KINYUA BIN KING’ORI: Wanasiasa wajiepushe na mjadala wa kuahirisha uchaguzi

Na KINYUA BIN KING’ORI

INGAWA Mahakama ya Afrika ilitoa ushauri kwamba mataifa ya bara hili ambayo huenda yatashindwa kuandaa uchaguzi mkuu kwa sababu ya makali ya janga la virusi vya corona, yanaweza kuzingatia kuahirisha shughuli hiyo, hilo linawezekana tu ikiwa sheria za kitaifa zinakubali uahirishaji wa uchaguzi.

Kwa rai hiyo, lazima katiba ya nchi husika ifanye hivyo. Sasa viongozi wa kisiasa wameanza kutumia muda wao mwingi kulumbana juu ya maoni hayo, wameingiza siasa mapendekezo ya mahakama hiyo.

Lakini ikiwa hawatokoma, watapotosha umma kipindi hiki cha ugumu wa maisha. Inavunja moyo kusikia baadhi ya viongozi hasa wa mrengo fulani wa kisiasa wakizungumza kauli zinazoweza kuvuruga usalama na umoja wetu wakati huu tunapoelekea kipindi cha kampeni mwaka 2022.

Siasa si lazima wanasiasa wapotoshe wananchi, wanapaswa kuwa wajasiri kuelezea ukweli katika mijadala yao kisiasa. Wanaotumia nafasi yao kuendesha porojo na propaganda wanafaa kuwa wa kwanza kuchujwa katika uchaguzi mkuu ujao wa 2022.

Tukizingatia maoni ya majaji wa korti ya Afrika, sijui kwa nini baadhi ya viongozi wetu wameanza kuhisi mchecheto kwenye matumbo yao. Maoni ya korti hiyo yalichapishwa kwa lugha ya wastani ili yaweze kueleweka kwa urahisi na kwa nia njema kwa mataifa yote ya Afrika na ulimwenguni kwa jumla.

Walisisitiza wazi ikiwa taifa fulani, tuseme mfano Kenya, linaweza kuahirisha uchaguzi mkuu ujao wa 2022, ikiwa kutakuwa sababu ya kueleweka inayotokana na janga la corona, lakini lazima katiba tunayoitumia iwe inacho kipengele kinachoruhusu uahirishaji huo.

Tukizingatia katiba yetu ya 2010, uchaguzi mkuu hufanyika Jumanne ya pili ya Agosti, kila baada ya miaka mitano. Kenya inaeleweka wazi uchaguzi mkuu utafanyika siku ya Jumanne, Agosti 9 mwaka wa 2022 na hilo Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka nchini (IEBC) imethibitisha mara si moja kila wanapoulizwa na vyombo vya habari.

Tukirejelea katiba yetu, haisemi maradhi au janga la njaa linaweza kuchangia uchaguzi mkuu kuahirishwa. Uchaguzi mkuu nchini Kenya waweza kuahirishwa tu ikiwa taifa letu (Kenya) litakuwa katika vita na taifa lingine au mataifa mengine.

Aidha, kubadilsha tarehe ya uchaguzi mkuu lazima Wakenya wenyewe wakubali kwa kubadilsha katiba na kufamyia mageuzi kipengele hicho, na hilo kutimizwa lazima tufanye hivyo kupitia kura ya maoni.

Ingawa si Mara ya Kwanza Kwa viongozi wetu kuzungumzia swala la uchaguzi mkuu kuahirishwa nchini, mazungumzo na kauli wanazotoa Kwa Sasa zimeanza kutia wakenya hofu na wengine kuanza kusadiki kweli huenda njama za kuchelewesha uchaguzi mkuu wa 2022 zikafaulishwa na serikali.

Wanaojifanya kupinga siku ya uchaguzi wa 2022 kubadilshwa hata nukta moja wacha sekondi au dakika, wanajitanua vifua wakisema watawasilisha barua kwa Baraza la usalama katika umoja wa mataifa (UN) kuelezea Kenya haiko vitani na lazima serikali iwe na mikakati bora kufanikisha zoezi la uchaguzi mkuu Kwa mujibu wa katiba.

Katika muktadha huo, ndio nauliza je, kwa nini viongozi watake kuvuruga maisha ya wananchi Kwa kuwasababishia hofu na uoga bure juu ya uchaguzi mkuu? Je, viongozi hao wanajua kuwatia raia hofu ni sawa kuwachochea kujiandaa kwa ghasia? , Je, wanao ushahidi upi kwamba kuna njama ya kuahirisha uchaguzi ujao?

 

You can share this post!

TAHARIRI: Tuchague viongozi kwa msingi wa sera

KAMAU: Kuna ishara ghasia za 2007/08 zitatokea tena