• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Vijana wataka vyuo vya kiufundi vianzishe masomo ya kidijitali

Vijana wataka vyuo vya kiufundi vianzishe masomo ya kidijitali

Na STEPHEN ODUOR

VIJANA katika Kaunti ya Tana River, wametaka mafunzo ya kisasa yatolewe katika taasisi na vyuo vya kiufundi ili kushawishi wengi wao kujiunga navyo.

Kulingana nao, taasisi hizo huchukuliwa kuwa za watu waliofeli katika elimu za msingi kwa vile mafunzo yanayotolewa yamejikita katika mbinu za zamani za utendakazi ilhali jamii ya sasa ni ya kidijitali.

“Hakuna mtu ambaye angependa kujifunza mambo ambayo yamepitwa na wakati katika enzi hizi,” akasema kiongozi wa vijana, Bi Asha Shehe.

Alidai kuwa, baadhi ya vijana waliopokea mafunzo kuhusu masuala ya umeme waliamua kufanya kazi ya bodaboda baada ya kukosa ajira zilizolingana na masomo yao, huku wengine kama vile fundi wa mifereji wakikosa ajira kwa vile mbinu walizofunzwa zilipitwa na wakati.

Waziri wa Elimu katika kaunti hiyo, Bw Abbas Kunyo alisema utawala uliopo unazingatia masuala hayo na tayari kuna mikakati ambayo ilikuwa imeanza kutekelezwa.

Bw Kunyo alisema mojawapo ya mikakati iliyoanzishwa ni kuwapa wahadhiri mafunzo ya kidijitali, ndipo wawe na uwezo wa kufunza mbinu za kisasa za utendakazi.

“Ukweli ni kuwa idadi ya wanafunzi katika taasisi zetu imekuwa ikiongezeka katika miaka ya hivi majuzi ikilinganishwa na zamani. Katika miezi ijayo, mtashuhudia wenyewe kozi mpya ambazo tutaanzisha,” akasema.

You can share this post!

Wanaomezea mate ugavana waongezeka

Amerika yafungia Taliban pesa