• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 6:55 AM
Onyo kwa wanahabari kuhusu ripoti za kisiasa

Onyo kwa wanahabari kuhusu ripoti za kisiasa

Na WANDERI KAMAU

WANAHABARI au vyombo vya habari ambavyo vitaonyesha mapendeleo kwa baadhi ya mirengo ya kisiasa vitaadhibiwa vikali uchaguzi wa 2022 unapokaribia, lilionya jana Baraza la Vyombo vya Habari Kenya (MCK).

Baraza hilo lilisema limepokea malalamishi kutoka kwa baadhi ya viongozi na wananchi kuwa baadhi ya vyombo vya habari vimekuwa vikionyesha mapendeleo ya wazi kwa mirengo fulani ya kisiasa, licha ya hilo kuwa kinyume cha kanuni za uanahabari.

Kwenye uzinduzi wa Jopo Maalum litakalobuni mwongozo utakaozingatiwa na vyombo vya habari kwenye uchaguzi huo, Afisa Mkuu Mtendaji wa baraza hilo, Bw David Omwoyo, alisema wakati umefika kwa sekta ya uanahabari kuwajibikia vitendo vyake.

Aliwatahadharisha wadau katika sekta hiyo kufahamu kuwa vitendo vyao vinaweza kuijenga ama kuibomoa nchi, kulingana na taratibu watakazofuata katika kuangazia masuala ya uchaguzi mkuu.

“Lazima tufahamu kuwa Wakenya wote watakuwa wameelekeza macho yote kwetu kufuatilia masuala yanayohusiana na uchaguzi mkuu wa mwaka ujao. Ili kuhakikisha tumewafahamisha matukio yote ifaavyo, lazima tuchukue hatua za mapema kuhakikisha kuna mwongozo wa pamoja utakaozingatiwa na kila mmoja katika sekta hii,” akasema Bw Omwoyo.

Alirejelea chaguzi za 2013 na 2017, ambapo baraza lilipokea visa vingi vya wanahabari kushambuliwa au vyombo vya habari kususiwa na baadhi ya Wakenya kwa tuhuma za kuegemea mirengo fulani ya kisiasa.

Kufuatia ghasia za baada ya uchaguzi tata wa 2007, vyombo vya habari vililaumiwa pakubwa kwa kuchangia hali hiyo, hasa vituo vya redio vinayotangaza kwa lugha asili.

Tafiti kadhaa pia zimevilaumu vituo hivyo kuwa kueneza ghasia na taharuki za kisiasa nchini.Bw Omwoyo alisema mwongozo huo unalenga kubuni mazingira ya wazi kwa vyombo hivyo kurejelea taratibu vinavyopaswa kuzingatia kabla ya kutangaza au kuandika masuala yanayohusiana na siasa za uchaguzi.

“Kama macho ya wananchi, jukumu letu linapaswa kuwafahamisha yanayojiri wala si kuendeleza ajenda za wanasiasa ama mirengo ya kisiasa,” akasema Bw Omwoyo.

Jopo linawashirikisha wanachama 21 kutoka vitengo mbalimbali vya sekta ya uanahabari na limepewa muda wa siku 20 kukamilisha kuandaa rasimu ya mwongozo huo.

Linaongozwa na Bw Joseph Odindo, ambaye aliwahi kuhudumu kama Mhariri Mkuu katika mashirika ya habari ya Nation (NMG) na Standard Group.

Baadhi ya wanachama wake ni Prof George Nyabuga, Bw Bernard Mwinzi (Mhariri Mkuu wa magazeti ya Saturday Nation na Sunday Nation), Bi Njeri Rugene kati ya wengine.

Akihutubu kwenye kikao hicho, Bw Odindo alisema watafanya kila wawezalo kubuni mwongozo bora ambao unalingana na mazingira ya kisiasa wakati huu.

“Jukumu letu halitakuwa jipya, kwani tutarejelea miongozo sawa iliyotumika mnamo 2013 na 2017. Hata hivyo, lengo kuu ni kuimarisha miongozo hiyo ili kuwiana na hali ya sasa,” akasema.

Baada ya jopo kumaliza kuandaa rasimu hiyo, itakabidhiwa wataalamu wa masuala ya habari, siasa na uchaguzi ili kupitiwa na kuboreshwa zaidi.

Baada ya hilo, itazinduliwa rasmi na kukabidhiwa vyombo vya habari.

You can share this post!

Binti adai kupigwa sababu hajakeketwa

Kilio huku familia 800 zikibomolewa makazi