• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
TAHARIRI: Heko chipukizi kuitawala dunia

TAHARIRI: Heko chipukizi kuitawala dunia

KITENGO CHA UHARIRI

KUKAMILIKA kwa mashindano ya vijana wasiozidi umri wa miaka 20 kumerejesha tabasamu nyusoni mwa Wakenya.

Mashindano hayo yaliyoandaliwa humu nchini na kuyaleta pamoja mataifa ya ulimwengu, yamedhihirishia dunia kwamba Kenya ingali hodari katika riadha.

Kinyume na mambo yalivyokuwa kwenye Olimpiki jijini Tokyo, Japan, chipukizi wetu walijikakamua na kumaliza katika nafasi ya kwanza.

Vijana hao walizoa jumla ya nishani tisa za dhahabu, moja ya fedha na saba za shaba.

Kivumbi hicho kilifanyika kwa mara ya kwanza barani Afrika na mataifa hodari kama vile Jamaica, Ethiopia, Botswana, Uganda kati ya mengine, hayakuwa na chao mbele ya chipukizi wetu.

Labda wasiotupenda watasema kwa kuwa mcheza kwao hutuzwa, vijana wetu walistahili kushinda. Huo si ukweli.

Ushindani uliotoka kwa nchi mbalimbali, ulionyesha kuwa hapakuwa na suala la vijana wetu kuwa kwao nyumbani.

Walijitolea na kupambana, hasa walipokaribia kwenye utepe.Mafanikio haya yanatuonyesha kuwa tunapofanya maandalizi mazuri na tukaweka malengo yetu ipasavyo, hakuna linalotushinda.

Vijana hao wametuletea fahari kama taifa. Walipokuwa wakishinda na wimbo wetu wa taifa ukiimbwa, mara moja tulisahau tofauti zetu za kisiasa na kudondokwa na machozi ya furaha.

Michezo ni kiungo muhimu katika kuwaleta watu pamoja, kujenga undugu wa kweli na kumaliza tofauti ndogo ndogo.

Wizara ya Michezo chini ya waziri Amina Mohammed inapaswa kushirikiana na ile ya Elimu, kutambua vipaji vingi katika shule za msingi na upili.

Ingawa janga la Corona limesimamisha michezo katika shule zetu, wadau wa wizara za Elimu, Michezo na Afya wanapaswa kutafuta mbinu za kuendeleza mashindano shuleni.

Wakufunzi, bila ya ubaguzi au mapendeleo, wazunguko katika kaunti zote 47 kutambua vijana walio na vipaji katika riadha pamoja na michezo mingine.

Kufanyika kwa mashindano haya katika Uwanja wa Kimataifa wa Kasarani bila shaka kumetoa fursa kwa ulimwengu kuona viwanja vyetu.

Serikali iendeleze ujenzi wa viwanja vyenye hadhi ya kimataifa kama cha Kasarani, ili siku za usoni tuandae mashindano makubwa kama Olimpiki na hata Kombe la Dunia.

You can share this post!

Familia moja Gatuanyaga yaomba msaada baada ya jamaa wao...

Serge Gnabry awabeba Bayern Munich dhidi ya Cologne kwenye...