• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
ONYANGO: Makamishna wa IEBC wasisimamie zaidi ya uchaguzi mmoja

ONYANGO: Makamishna wa IEBC wasisimamie zaidi ya uchaguzi mmoja

Na LEONARD ONYANGO

SHERIA inafaa kufanyiwa marekebisho kuhakikisha kuwa makamishna wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) hawaruhusiwi kusimamia zaidi ya uchaguzi mmoja.

Hatua hiyo itahakikisha kuwa Wakenya wanakuwa na imani na tume ya IEBC katika Uchaguzi Mkuu wa Agosti 9, 2022.

Kila wakati wa uchaguzi mkuu Wakenya wamekuwa wakiishi kwa taharuki kutokana na hofu ya kutokea kwa vurugu.

Fujo hizo zinasababishwa na Wakenya kukosa imani na tume ya IEBC.

Uchaguzi huru na wa haki ndio dawa ya kumaliza fujo ambazo zimekuwa zikishuhudiwa kila mara baada ya uchaguzi.

Tayari viongozi wa ODM wakiongozwa na mwenyekiti wake wa kitaifa Bw John Mbadi, wamemtaka mwenyekiti wa IEBC Wafula Chebukati kujiuzulu ili kuachia kikosi kipya shughuli ya usimamizi wa uchaguzi mkuu ujao.

Bw Chebukati pamoja na makamishna Bw Abdi Guliye na Bw Boya Molu walisimamia uchaguzi mkuu wa 2017 na sasa watasimamia tena uchaguzi wa 2022.

Watatu hao wanatarajiwa kustaafu Januari 20, 2023.

Makamishna wapya Bi Juliana Cherera, Bw Francis Wanderi, Bi Irene Masit na Bw Justus Nyang’aya, walioapishwa wiki iliyopita, pia watasimamia uchaguzi mkuu wa 2022 na 2027 na watastaafu Septemba 2, 2027.

Hiyo inamaanisha kwamba iwapo matokeo ya urais wa uchaguzi mkuu wa 2027 yatabatilishwa na Mahakama ya Juu, wanne hao hawataandaa kwani watakuwa wameondoka.

Kwa mujibu wa Katiba, uchaguzi wa marudio wa urais baada ya matokeo kubatilishwa na Mahakama ya Juu, unafaa kuandaliwa ndani ya siku 60.

Bw Chebukati pamoja na makamishna wenzake wawili, hawafai kusimamia Uchaguzi Mkuu ujao kwani imani ya Wakenya kwao ni imedorora mno.

Kubatilishwa kwa matokeo ya urais ya uchaguzi wa Agosti 8, 2017 kulitia doa Bw Chebukati na makamishna wenzake.

Kadhalika, barua iliyoandikwa na Bw Chebukati baada ya Mahakama ya Juu kubatilisha matokeo ya urais 2017 ni ishara kwamba, watatu hao hawakutekeleza majukumu yao vyema.

Bw Chebukati katika barua yake kwa aliyekuwa Afisa Mtendaji wa IEBC Ezra Chiloba, kwa mfano, alitaka kujua kwa nini vifaa vya kielektroniki vya kutambua wapigakura na kupeperusha matokeo (KIEMS) vilifeli siku ya uchaguzi.

Bw Chebukati pia alitaka kufahamishwa kwa nini simu za setelaiti zilizogharimu Sh848 milioni, hazikutumiwa siku ya uchaguzi.

Hiyo inamaanisha kuwa makamishna hao waliachia sekretariati ya IEBC kuendesha shughuli zote za uchaguzi na hawakujua kilichokuwa kikiendelea.

Bw Chebukati hajajitokeza kueleza Wakenya kuhusu hatua ambazo zimevchukuliwa na tume hiyo kuzuia makosa ya aina hiyo.

You can share this post!

Farouk Shikhalo asajiliwa na KMC ya Tanzania

Wito viongozi wa kisiasa wasitishe kampeni za mapema